Na A.O. Ali
Kampuni mashuhuri ya filamu ya Banyak kutoka nchini Uingereza, imetangaza nia na dhamira yake ya kufanya kazi pamoja na kampuni ya Rafiki Network  nchini Tanzania katika kufanikisha tukio lake la kwanza la resi ndefu za ngalawa litakalofanyika tarehe 18 Disemba, 2016, huko Vumawimbi kisiwani Pemba visiwani Zanzibar.
Akitoa taarifa huyo kwa mwandishi wa habari hii kupitia mazungumzo ya simu, Rais wa kampuni ya Rafiki Network Bwana Hamad Omar Hamad amethibitisha kuwa mazungumzo kati yao na kampuni ya Banyak yameshakamilika na kwa sasa kampuni hiyo inakamilisha utaratibu wa kujiandaa kwa ajili ya tukio hilo.
“ Napenda niwahakikishie kuwa baada ya kuliona wazo letu hili la kutaka kuanzisha resi  ndefu za ngalawa hapa Afrika Mashariki, wenzetu wa BANYAK wa kule Uingereza hawakufikiri mara mbili. Wamesema wako tayari kuja nchini kushirikiana nasi kikamilifu.”  Alisema Bwana Hamad.
Aidha Bwana Hamad amesema amefarijika sana kuwa licha ya kuwasiliana na wadau wengi wa biashara yakiwamo mashirika ya simu, ndege na usafiri wa baharini, imempa moyo sana kuona kwamba kampuni hii ya kigeni ndiyo imekuwa ya kwanza kuona fursa adhimu na kujitokeza kushiriki katika tukio hili adhimu na la kihistoria nchini.
“ Wenzetu wa Banyak hawakujali tukio hili linaandaliwa na nani, wapi na vipi. Baada ya kuona baadhi ya maandiko  na posta ya tangazo la tukio letu, imewatosha wao kuona kuwa kuna fursa kubwa katika tukio hili. Kwa kutambua umhimu wa tukio lenyewe wameamua kuchukua gharama na muda wao kuja kushiriki kikamilifu katika kufanikisha tukio letu hili. Kwa kweli ni habari njema sana kwetu!” Alisema Bwana Hamad.
Kampuni ya Banyak ni moja kati ya kampuni mashuhuri nchini Uingereza ambayo kwa muda mrefu imekuwa ikijishughulisha na kuandaa makala za video (documentary) zenye kuelimisha  jamii. Kampuni hiyo yenye makazi yake jijini London, itaingia makubaliano ya kurikodi tukio zima la resi za ngalawa zitakazofanika Pemba mwishoni mwa mwaka huu. Resi hizo ndefu zaidi kuwahi kutokea katika pwani ya Afrika Mashariki zitaanzia bandari ya Vuma wimbi na kuishia bandari ya Tumbe, takribani mwendo wa kilomita 30 za baharini.
Resi hizo zitashirikisha Ngalawa kutoka maeneo mbali mbali ya Tanzania sambamba na kuwashirikishi kikamilifu wamiliki wa ngalawa kutoka maeneo enyeji ya Tumbe, Shumba mjini, Kiuyu, Msuka, Tondooni na kwengineko ambapo ngalawa kati ya 30 hadi 50 zitashiriki.
Kampuni ya Rafiki Network imeanzishwa mwaka 2016 na kusajiliwa visiwani Zanzibar ambapo miongoni mwa kazi zake ni kuandaa matukio mbali mbai ya Elimu na Utamaduni kwa lengo la kuiwezesha jamii kimaisha kwa kufungua milango ya fursa za ajira sambamba na kukuza utalii wa ndani na wa nje hapa nchini.
Resi hizi za Ngalawa ndio tukio la mwanzo kubwa kuandliwa na Kampuni ya Rafiki Network ambapo wadau mbali mbali kama ZANTEL, TIGO, HALOTEL, ZSSF, Vigor Group of Companies, TASAKHTA Hospitals na Sun Tours zimeombwa kudhamini tukio hili. Kampuni nyengine ni Hotel ya Tembo, Serena na nyenginezo ambapo pia mashirika mbali mbali ya ndege pia yameombwa  kutoa udhamini.
“ Kwa hakika tuna tamaa kubwa ya kupata mashirikiano na wadhamini wetu. Hadi sasa TASAKHTA Hospital na Sun Tours wamejitokeza rasmi kudhamini sehemu ya tukio hili. Hata hivyo tunawakaribisha wadhamini wengine waweze kuiona fursa iliyopo mbele yao na wajitokeze kudhamini tukio hili lenye manufaa kwao na jamii kwa ujumla.” Bwana Hamad Omar alitoa wito sambamba na kuushukuru Uongozi wa Hospitali ya TASAKHTA na Kapmuni nguli ya utalii visiwani Zanzibar ya SUN Tours kwa kukubali kushiriki na kudhamini sehemu ya tukio hili.

Tukio hili sambamba na kudhaminiwa na mashirika mbali mbali linatarajiwa kuhudhuriwa na vyombo mbali mbali vya habari vya ndani na nje ya nchi ambapo idadi kubwa ya wageni na washabiki inatarajiwa pia kujitokeza kwa wingi kujionea tukio hili la kihistoria katika nchi yetu.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...