Na Felix Mwagara, MOHA
SERIKALI kwa kushirikiana na Mashirika ya Kimataifa wameanza kujadili nyenzo mbalimbali ambazo zitasaidia kuwalinda na kuwasaidia watoto walioathirika na biashara ya kusafirisha binadamu nchini.

Akizungumza wakati akifungua warsha ya siku mbili ya kujadili jinsi ya kuwalinda na kuwasaidia watoto walioathirika na biashara ya kusafirisha binadamu, inayofanyika katika Ukumbi wa Mikutano, Hoteli ya Hyatt Regency jijini Dar es Salaam leo, Katibu wa Sekretarieti ya Kitaifa ya Kuzuia na Kupambana na Biashara Haramu ya Binadamu kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Separatus Fella alisema warsha hiyo ni muhimu ikiwa na lengo la kusaidia idadi kubwa ya watoto walioathirika nchini.

Alisema Tanzania ambayo ni kati ya mataifa yanayoshamiri kwa biashara haramu ya kusafirisha watoto kwa lengo la kwenda kuwatumikisha kazi katika maeneo mbalimbali nchini pamoja na duniani kwa ujumla, kupitia nyenzo hizo zitakazo jadiliwa zitasaidia kutoa elimu kwa umma juu ya matatizo hayo nchini.
“Nyenzo hizi za kuwasaidia na kuwalinda wale watoto walioathirika baada ya kutoka katika maeneo mbalimbali zitasaidia kutoa elimu ya kuwandaa kisaikolojia ili wasikate tamaa na maisha, pia watoto watalindwa na baadaye watarudishwa kwa wazazi wao ili waweze kuendelea majukumu mengine ya kujenga taifa,” alisema Fella na kuongeza;
“Kumekuwepo na wimbi kubwa la kuwasafirisha wasichana wa Kitanzania kwenda nchi za uarabuni kwa lengo la kwenda kufanya kazi za ndani, ila wanapofika huko mambo yanawaharibikia wanaanza kudhalilishwa, kunyanyaswa kiasi kwamba wanashindwa kupata misaada, kutokana na manyanyaso hayo urudi nchini wakiwa wameathirika kwa kiasi kikubwa.”
Fella alisema wadau wa warsha hiyo watatoa elimu kwa umma kuhusu kukomeshwa kwa biashara hiyo haramu na wazazi kutokuwaruhusu watoto wao kwenda kufanyiwa unyanyasaji huo kwa kuwa ni kinyume cha sheria. Hata hivyo, kutokana na wimbi hilo kuzidi kushika kasi nchini, pia wadau hao watatoa elimu ya watoto walioathirika mara baada ya kurudi nchini ili wajitambue kutokana na mateso mbalimbali waliokumbana nayo ili wasiweze kukata tama kutokana na vitendo vya ukatili walivyofanyiwa katika maeneo wanayotoka.
Aidha, Mwakilishi Mkuu wa Umoja wa Ulaya (EU) upande wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla, Balozi Roeland Van de Geer alisema Tanzania ni kati ya nchi zilizoathirika na biashara haramu ya kusafirisha watoto, hivyo elimu inahitajika ili kukomesha biashara hii hatari.
“Watoto wa leo ni mabibi na mabwana wa kesho, hivyo wapaswa kulindwa pamoja na kuelimishwa, Umoja wa Ulaya utaendelea kushirikiana na Tanzania katika kuwasaidia watoto waweze kuepuka mateso wanayoyapata,” alisema Roeland.
Warsha hiyo iliandaliwa na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na kufadhiliwa na Umoja wa Ulaya pamoja na Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) na inatarajiwa kumalizika Oktoba 20 mwezi huu ambapo wadau hao wataanza kufanyia kazi nyenzo hizo zilizojadiliwa.
Mwakilishi Mkuu wa Umoja wa Ulaya (EU) upande wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla, Balozi Roeland Van de Geer akitoa hotuba yake katika Warsha ya siku mbili ya kujadili jinsi ya kuwalinda na kuwasaidia watoto walioathirika na biashara ya kusafirisha binadamu nchini. Katikati ni Katibu wa Sekretarieti ya Kitaifa ya Kuzuia na Kupambana na Biashara Haramu ya Binadamu kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Separatus Fella, na kulia ni Mratibu wa Mradi wa Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM), Tamara Keating. Warsha hiyo inafanyika katika Hoteli ya Hyatt Regency, jijini Dar es Salaam. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Katibu wa Sekretarieti ya Kitaifa ya Kuzuia na Kupambana na Biashara Haramu ya Binadamu kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Separatus Fella (wapili kulia-meza kuu), akitoa hotuba ya ufunguzi wa Warsha ya Siku mbili ya kujadili jinsi ya kuwalinda na kuwasaidia watoto walioathirika na biashara ya kusafirisha binadamu. Fella alisema wadau wa warsha hiyo watatoa elimu kwa umma jinsi ya kuwasaidia idadi kubwa ya watoto ambao wameathirika. Wapili kushoto meza kuu ni Mwakilishi Mkuu wa Umoja wa Ulaya (EU) upande wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla, Balozi Roeland Van de Geer. Kushoto ni Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) nchini, Dr Qasim Sufi, na kulia ni Mratibu wa Mradi wa Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM), Tamara Keating. Warsha hiyo inafanyika katika Hoteli ya Hyatt Regency, jijini Dar es Salaam. Picha zote na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
Katibu wa Sekretarieti ya Kitaifa ya Kuzuia na Kupambana na Biashara Haramu ya Binadamu kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Separatus Fella (katikati), akiteta jambo na Mwakilishi Mkuu wa Umoja wa Ulaya (EU) upande wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla, Balozi Roeland Van de Geer, mara baada ya Katibu huyo kufungua Warsha ya siku mbili ya kujadili jinsi ya kuwalinda na kuwasaidia watoto walioathirika na biashara ya kusafirisha binadamu nchini. Fella alisema baada ya warsha hiyo, washiriki hao wataanza kutoa elimu kwa umma jinsi ya kuwasaidia idadi kubwa ya watoto ambao wameathirika. Kushoto ni Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) nchini, Dr Qasim Sufi. Warsha hiyo inafanyika katika Hoteli ya Hyatt Regency, jijini Dar es Salaam. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
Katibu wa Sekretarieti ya Kitaifa ya Kuzuia na Kupambana na Biashara Haramu ya Binadamu kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Separatus Fella (wapili kulia-waliokaa), Mwakilishi Mkuu wa Umoja wa Ulaya (EU) upande wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla, Balozi Roeland Van de Geer (wapili kushoto-waliokaa), Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) nchini, Dr Qasim Sufi (kushoto-waliokaa), Meneja wa Mradi Umoja wa Ulaya (EU), Anna Costantini, wakiwa katika picha ya pamoja na wadau kutoka Taasisi za Serikali pamoja na Mashirika yasiyokuwa ya Serikali, mara baada ya kufunguliwa warsha ya siku mbili ya kujadili namna ya kuwalinda na kuwasaidia watoto walioathirika na biashara ya kusafirisha binadamu nchini. Warsha hiyo inafanyika katika Hoteli ya Hyatt Regency, jijini Dar es Salaam. 
Picha zote na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...