Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kuuwawa kwa watafiti watatu (3) wakiwa kazini, tukio lililotokea Oktoba mosi mwaka huu katika kijiji cha Iringa-Mvumi, Wilayani Chamwino, Mkoa wa Dodoma.

Tume inalaani vikali mauaji haya ya kikatili ya watu wasiokuwa na hatia na yenye kuitia aibu nchi yetu. Aidha, inaungana na watanzania wengine nchini kuwapa pole wafiwa na wote walioguswa na msiba huu.

Kwa mujibu wa taarifa za vyombo vya habari watafiti hao kutoka Chuo cha Utafiti wa Udongo na Maendeleo ya Ardhi cha Selian, Arusha wakiwa kijijini hapo kukusanya sampuli za udongo kwa ajili ya utafiti walivamiwa na kundi la wanakijiji na kushambuliwa kwa mapanga na silaha za jadi na kisha kuchomwa moto kwa imani kwamba eti walikuwa wanyonya damu. 

Haki ya kuishi kama zilivyo haki nyingine, inalindwa na sheria na hakuna mtu anayepaswa kuporwa haki hii ya msingi kiholela. Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 14, kila mtu anayo haki ya kuishi na kupata kutoka katika jamii hifadhi ya maisha yake, kwa mujibu wa sheria. 

Pia Mikataba mbalimbali ya kimataifa na kikanda ambayo Tanzania imeridhia inatoa ulinzi juu ya haki ya mtu kuishi. Baadhi ya Mikataba hiyo ni: Azimio la Kimataifa la Haki za Binadamu la 1948 (Kifungu cha 3) na Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa wa 1966 (Kifungu cha 6) vinavyoeleza kuwa kila mtu anayo haki ya asili ya kuishi, inayolindwa kisheria na hakuna atakayenyimwa haki hii ya msingi kiholela.

Hivyo kuuwawa kwa watafiti hao wakiwa katika utekelezaji wa majukumu yao kwa taifa ni kitendo kinachopaswa kulaaniwa vikali na kila mwananchi anayethamini uhai na kuheshimu haki za binadamu.

Kumbukumbu zinaonyesha kuwa matukio ya wananchi kujichukulia sheria mikononi mwao ni jambo linalojirudiarudia na limekuwa likisababisha uvunjifu wa haki za binadamu na madhara makubwa kwa jamii, hususan kwa wanawake na watoto.

KUSOMA ZAIDI BOFYA HAPA

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...