Na Hilali A. Ruhundwa- COSTECH
Serikali za Finland na Tanzania kupitia Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) zimekubaliana kuendeleza sekta ya ubunifu (innovation) kupitia mradi wa TANZIS utakaogharimu zaidi ya shilingi bilioni 28 kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwakani 2017.
Hayo yamebainika jana wakati Waziri wa Biashara za Nje na Maendeleo wa Finland Bw. Kai Mykkänen na ujumbe wake walipotembelea COSTECH katika maadhimisho ya kukamilika kwa mradi wa miaka mitano wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) uliojulikana kama The Information Society and ICT Sector Development Project in Tanzania (TANZICT).
Bw. Mykkänen alisema amefurahishwa na jinsi mradi wa kwanza ulivyofanikiwa kwa kuendeleza vijana wabunifu zaidi ya 5,000 chini ya kitengo cha ubunifu (Buni Innovation Hub) kinachosimamiwa na COSTECH.
Waziri wa Biashara za Nje na Maendeleo wa Finland Bw. Kai Mykkänen akielezea ushirikiano wa Finland na Tanzania katika kuendeleza Teknolojia na Ubunifu.
“Tunafurahi kwa ushirikiano huu wa Tanzania na Finland hasa katika kuendeleza sekta ya teknolojia ya habari na mawasiliano kwa vijana wabubifu wa kitanzania. TANZICT imefanikiwa kwa kiasi kikubwa. Baada ya mradi huu, tunategemea kuwa na mradi mpya kuanzia mwaka kesho”. Alisema waziri huyo aliyeambatana na balozi wa nchi hiyo hapa nchini Pekka Hukka.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH Dr. Hassan Mshinda, alisema kutokana na tatizo la ukosefu wa ajira nchini, mradi huo ulijikita zaidi katika kuendeleza ubunifu wa vijana wanaohitimu vyuo vikuu na vyuo vishiriki katika kuwaendeleza na kuwajengea maarifa ili waweze kumudu soko la ushindani wa ajira.
Meneja wa Buni Innovation Hub Bw. Jumanne Mtambalike akiwasilisha mafanikio ya mradi wa TANZICT mbele ya ujumbe toka Finland.
“Katika mradi huu mpya utakaoanza mwaka kesho, utajikita zaidi katika sekta za viwanda, kilimo na afya lengo zaidi ikiwa ni kuimarisha uchumi wa nchi na kuongeza masoko ya bidhaa”. Aliongeza Dr. Mshinda.
Kwa upande wake Meneja wa BuniHub Bw. Jumanne Mtambalike, alisema mradi huo umekuwa mkombozi mkubwa kwa vijana wabunifu ambao umewawezesha wahitimu wa vyuo kuanzisha kampuni zao na kujiajiri.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...