Benjamin Sawe-Maelezo.
Serikali imesema pamoja na umuhimu wa
kilimo bado kuna changamoto ya kuwa na data za kuaminika kwa uundaji,
ufuatiliaji na utekelezaji wa sera za kilimo.
Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu Wizara ya
Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Dk. Florens Turuka leo jijini Dar es salaam alipofungua
warsha ya siku tano iliyowashirikisha wawakilishi kutoka nchi 25 Barani Afrika
ambao utajadili namna ya kuweka mikakati itakayowawezesha kupata data sahihi za
kilimo.
“Bado tuna tatizo la Data au Takwimu
ambazo tunaweza kuwa na uhakika nazo, hivyo wenzetu wameamua kuweka mikakati itakayosaidia
nchi za Afrika kukusanya Data zitakazosaidia
kufanya maamuzi katika sekta ya kilimo na maendeleo vijijini” alisema.
Alisema kilimo kinachangia asilimia 35 ya pato la taifa na asilimia 70 ya
ajira na ukuaji wa kila mwaka wa kilimo unatarajiwa kukua kwa asilimia 4.
Wakati huohuo, Meneja wa Takwimu za Kilimo Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Titus
Mwisomba alisema bila takwimu hizo hawawezi kupima maendeleo waliyofikia hasa
kwa upande wa sekta ya kilimo.
Alisema Ofisi ya Taifa ya Takwimu wamejipanga kutumia teknolojia ya kisasa
zikiwemo simu za mkononi ili kupata takwimu kwa haraka na kwa wakati sambamba
na kupunguza gharama za uendeshaji wa tafiti mbalimbali nchini.
Alizitaja changamoto zinazowakabili ni pamoja na upatikanaji wa wataalam wa
ukusanyaji wa takwimu ambapo tayari wameanza kutoa mfunzo kupitia Chuo cha
Afrika Mashariki cha Takwimu ili kukabiliana na changamoto hiyo.
Mbali na kuwashirikisha wataalam mbalimbali, mkutano huo pia
uliwashirikisha wataalamu kutoka Shirika la Chakula na Kilimo Duniani(FAO) pamoja
na Benki ya Maendeleo ya Afrika(AfDB).
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi Sekta ya Kilimo Dkt. FlorensTuruka akizindua Warsha ya siku Tano ya Kukusanya Takwimu Sahihi Zinazotokana na Kilimo Barani Afrika, Warsha hiyo imeshirikisha jumla ya nchi 25 na imefunguliwa jijini Dar es Salaam leo.
Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Dr. Albina Chuwa akiongea na washiriki wa Warsha ya Siku Tano ya Kukusanya Takwimu Sahihi Zinazotokana na Kilimo Barani Afrika, Warsha hiyo imeshirikisha jumla ya nchi 25 na imefunguliwa jijini Dar es Salaam leo.
Baadhi ya Washiriki wa Warsha ya kukusanya Takwimu Sahihi zinazotokana na Kilimo Barani Afrika wakimsikiliza Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi Sekta ya Kilimo Dkt. Florens Turuka (hayupo pichani) wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo uliofanyika jijini Dar es Salaam leo.
Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika Tanzania Dkt. Tonia Kandiero akiongea katika uzinduzi wa Warsha ya Siku Tano ya Kukusanya Takwimu Sahihi Zinazotokana na Kilimo Barani Afrika. (Picha na Benjamin Sawe-Maelezo)
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...