Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Katika Umoja wa Mataifa Balozi Tuvako Manongi akiwa na Profesa Chris Maina Peter aliyesimama pamoja na baadhi ya Maofisa wa Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania mara baada ya kutangazwa kwa majina ya wagombea 34 ambao walishinda kwa kupigiwa kura ya siri na Wajumbe wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuwa wajumbe wa Tume ya Kimataifa ya Sheria ( ILC) katika uchaguzi uliofanyika jana ( alhamisi) hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York, Marekani.
Bi. Lilian Mukasa ,Afisa wa Uwakilishi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa ambaye pia anahusika na masuala ya Uchaguzi ( Election Officer) akiwapigia kura wagombea ambao wameomba kuwa wajumbe wa Tume ya Kimataifa ya Sheria. Nyuma anaonekana Mgombea wa Tanzania, Profesa Chris Maina Peter ambaye alishindana na wagombea wengine 13 kutoka Afrika ambapo walitakiwa nane kati ya hao 13. Afisa Lilian kwa nafasi yake kama Election Officer alikuwa na jukumu kubwa la kusaidia na kufanikisha mgombea wa Tanzania anapata kura za kutosha.
Na Mwandishi Maalum, New York
Profesa Chris Maina Peter , kutoka Tanzania, ni kati ya wagombea nane miongoni mwa wagombea 13 kutoka Afrika, ambao jana ( alhamisi ) Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa liliwapiga kura ya siri ya kuwachagua kuwa wajumbe wa Tume ya Kimataifa kuhusu masuala ya Sheria ( International Law Commission).
Ushindi wa Profesa Maina ambaye ataitumikia Tume hiyo wa miaka mingine mitano kuanzia Januari 2017, pamoja na juhudi zake binafsi za kujinadi, kujitangaza, kwa wajumbe 193 wa Baraza Kuu la Umoja wa Matifa, na akisheheni sifa na weledi mkubwa katika sheria za kimataifa. Ushindi wake umechangiwa zaidi na kazi kubwa iliyofanywa na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa Balozi Tuvako Manongi kwa kushirikiana na Maafisa wake ambao walifanya kazi kubwa ya kumkampenia na kumwombea kura.
Ingawa Profesa Maina anaingia kama mtu binafsi katika kazi za ILC anabeba jina na kuipeperusha bendera ya Tanzania katika Tume hiyo. Na kwa sababu hiyo, ushiriki wa Serikali katika kupendekeza jina lake pamoja na kumsaidia katika kampeni ilikuwa ni sehemu kubwa ya kufanikisha hatua hiyo muhimu ya kuendelea tena kuitumikia Tume kwa pindi cha pili cha miaka mitano.
Katika uchaguzi huo wa jana ambao ulikuwa na ushindani mkubwa huku ukishuhudia nchi kubwa kama Ufaransa ikishindwa kufurukuta. Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilitakiwa kuwachagua wajumbe 34 watakaohudumu katika Tume hiyo kwa mgawanyo wa wajumbe nane kutoka Afrika, wajumbe Saba kutoka Asia-Pacific , wajumbe wanne kutoka Ulaya ya Mashariki, wajumbe saba kutoka Amerika ya Kusini na Visiwa vya Caribbean na wajumbe nane kutoka nchi za Ulaya Magharibi na nchi nyingine.
Baada ya upigaji huo wa kura ya sira, washindi waliotangazwa kwa upande wa Afrika, waliochaguliwa ni Chris Maina Peter(Tanzania) Ahmed Laraba (Algeria), Tacouba Cissé (Ivory Coast), Dire D. Tladi (South Africa), Hussein A. Hassouna (Misri), S. Amos Wako (Kenya), Charles C. Jalloh (Sierra Leone) na Hassan Ouazzani Chahdi (Morocco).
Kutoka Asia-Pacific waliochaguliwa ni Ali bin Fetais Al-Marri (Qatar), Mahmoud Daifallah Hmoud (Jordan), Huikang Huang (China), Shinya Murase (Japan), Hong Thao Nguyen (Vietnam), Ki Gab Park (Jamhuri ya Korea ) na Aniruddha Rajput (India).
Waliochaguliwa kutoka Amerika ya Kusini na Caribbean ni Carlos Argüello Gómez (Nicaragua), Juan Manuel Gómez-Robledo (Mexico), Claudio Grossman Guiloff (Chile), Juan Jose Ruda Santolaria, (Peru), Gilberto Vergne Saboia (Brazil), Eduardo Valencia -Ospina (Colombia) na Marcelo Vázquez-Bermúdez (Ecuador).
Wajumbe kutoka Ulaya ya Mashariki waliochaguliwa ni Bogdan Aurescu (Romania), Kirumi Anatolyevitch Kolodkin, (Shirikisho la Urusi), Ernest Petric (Slovenia) na Pavel Šturma (Jamhuri ya Czech).
Kwa upande wa Ulaya Magharibi na nchi nyingine waliopita ni , Concepción Escobar Hernández (Hispania), Patrícia Galvão Teles (Portugal), Marja Lehto (Finland), Sean David Murphy (United States), Georg Nolte (Ujerumani), Nilufer Oral (Uturuki), Agosti Reinisch (Austria) na Michael Wood (United Kingdom).
Majukumu ya Tume ya Kimataifa kuhusu sheria pamoja na mambo mengine, ni kukuza na kuendeleza sheria za kimataifa, kutoa ushauri wa kitafiti kuhusu sheria mbalimbali, kupitia masuala yahusuyo sheria na mikataba ya kimataifa.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...