Na Bashir Nkoromo.
Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana
ameongoza mamia ya wananchi katika maziko ya muasisi wa chama cha
Tanganyika African Union (TANU) na baadaye Chama Cha Mapinduzi (CCM),
Khadija Kamba, aliyefariki juzi na kuzikwa jana katika makaburi ya
Kisutu jijini Dar es Salaam.
Kinana ambaye
alifuatana na Naibu Katibu Mkuu wa CCM-Bara, Rajab Luhwavi, akitoa salam
za zambirambi za Chama, alisema, CCM itamkumbuka na kuuenzi daima
mchango mkubwa alioutoa hasa wakati wa harakati za ujenzi wa TANU na
harakati za ukombozi wa Tanzania wakati wa uhai wake.
"Binti
Kamba alikuwa ni nguzo na chachu muhimu katika kuasisiwa kwa TANU na
mpambanaji aliyekuwa mstari wa mbele katika harakati za kutafuta Uhuru
wa nchi hii, hivyo Chama kitambukumbuka na kumuenzi daima Mama huyu",
alisema Kinana, wakati akitoa salam za rambirambi wakati wa maziko.
Kinana
alisema, licha ya kuwa muasisi, lakini Binti Kamba kamtika maisha yake,
aliendelea kuwa nwanachama na kada mwaminifu wa Chama Cha Mapinduzi na
kuendelea kuwa kisima cha kuchota hekima na maarifa hadi anafariki
dunia.
Alisema, kutokana na kuguswa na msiba
huo, kwa nafasi yake ya Katibu Mkuu wa Chama, ameandaa hitima
itakayosomwa keshokutwa katika Msikiti wa Masjid Quba, kumuombea
maghfira.
Binti Kamba, ambaye amefariki akiwa
na umri wa miaka 94, alifariki juzi asubuhi, nyumbani kwa mwanae wa
kulea, Kamba Abdallah, jijini Dar es Salaam.
Msafara
kwenda kwenye maziko Kisutu ulianzia nyumbani kwa marehemu, Ilala
Bungoni, Dar es Salaam, baada ya kuswaliwa, ambako miongoni mwa
waombolezaji waliokuwepo ni pamoja na Muasisi mwingine wa TANU Kingunge
Ngombale-Mwiru, ambaye mwaka jana alihamia Chadema kumfuata aliyekuwa
mgombea urais kwa tiketi ya Chama hicho Edward Lowassa.
Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana (kushoto) na Naibu Katibu Mkuu wa CCM-Bara Rajab Luhwavi, akishiriki kubeba jeneza lenye mwili wa Muasisi wa TANU, Khadija Kamba, katika makaburi ya Kisutu, wakati wa mazishi yaliyofanyika leo, Desemba 01, 2016, katika makaburi hayo mjini Dar es Salaam. (Picha na Bashir Nkoromo).
Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana akimwaga udogo kaburini wakati wa mazishi ya Muasisi wa TANU, Khadija Kamba, katika Makaburi ya Kisutu, Dar es Salaam, leo Desemba 01, 2016. Nyuma yake ni Naibu Katibu Mkuu wa CCM-Bara, Rajab Luhwavi. (Picha na Bashir Nkoromo).
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...