Na Anna Nkinda – JKCI.
1/12/2016 Mbunge wa Jimbo la Ilala Mhe. Azzan Musa Zungu amewashukuru wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) kwa huduma nzuri ya matibabu wanayompatia na kuiomba taasisi hiyo kutoa huduma kama hiyo kwa watanzania wote.
Mhe. Zungu ambaye amelazwa katika Taasisi hiyo amezitoa shukrani hizo leo wakati akiongea na waandishi wa habari waliotaka kufahamu kuhusu maendeleo ya afya yake.
“Namshukuru Mwenyezi Mungu naendelea vizuri hali yangu siyo kama jana. Nilianza kuumwa majira ya saa nane 8:30 mchana nikiwa nyumbani katika mazingira magumu ambapo mapigo ya moyo yalipanda ghafla nikapelekwa Hospitali ya Amana na baadaye Muhimbili kitengo cha Huduma ya dharula majira ya saa 12jioni kisha nikaletwa hapa”.
“Kwa namna ya pekee nawashukuru sana wafanyakazi wa Amana, Muhimbili na Taasisi ya Moyo ambao wamenipokea na kunipa huduma nzuri na kama mnavyoniona afya yangu inaendelea vizuri tofauti na nilivyokuja jana”. alisema Mhe. Zungu.
Aidha Mhe. Zungu aliwataka watanzania kujiunga na mfuko wa Taifa wa Bima ya afya ambao hata yeye ni mwanachama kwa kuwa mwanachama wa mfuko huu kutawasaidia kupata matibabu pindi watakapoumwa bila ya kutoa fedha mfukoni.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Prof. Mohamed Janabi alisema hali ya Mhe. Zungu inaendelea vizuri tofauti na walivyompokea jana. Hivi sasa madaktari wako katika uchunguzi wa matatizo ya Moyo baada ya hapo watajuwa tatizo na kumpatia tiba na anaamini baada ya siku tatu zijazo anaweza kuruhusiwa.
“Kipindi cha nyuma viongozi wenye matatizo kama haya walikuwa wanapelekwa nje ya nchi kwa ajili ya matibabu hivi sasa Serikali imeboresha huduma za matibabu ya Moyo hivyo basi wagonjwa wengi wanatibiwa hapa nchini”, alisema Prof. Janabi.
Aliwashauri wananchi kupima afya zao japo mara moja kwa mwaka, wakiona dalili za viashiria vya ugonjwa wa Moyo waende haraka Kituo cha Afya kilichopo jirani kwa ajili ya matibabu.
Prof. Janabi alimalizia kwa kuwasisitiza wananchi kufanya mazoezi na kula vyakula sahihi na kwa upande wa wagonjwa wa Moyo wanatakiwa kumeza dawa kipindi chote cha maisha yao wasiache kunywa dawa kwani wagonjwa wengi wanaorudi kupata matibabu ni wale walioacha kumeza dawa.
Mbunge wa Jimbo la Ilala Mhe. Azzan Musa Zungu akiwa amelazwa katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) kwa ajili ya kupatiwa matibabu ya moyo ambapo kwa sasa hali yake inaendelea vizuri. Kutoka kulia ni Muuguzi Mwandamizi Sr. Chagui Mgaza na kushoto ni Mwinyi Maulidi ambaye ni dereva wa Mhe. Zungu.Picha na Anna Nkinda - JKCI
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...