Na Eleuteri Mangi, WHUSM
Wakurugenzi wa halimashauri wameaswa kutumia fursa uwepo wa Chuo cha
Maendeleo ya Michezo Malya kilichopo mkoani Mwanza kwa kuwaruhusu walimu wa
michezo wengi zaidi kuongeza ujuzi wao ili kuinua sekta ya michezo nchini.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
Prof. Elisante Ole Gabriel alipotembelea chuo hicho kujionea namna chuo hicho
kinavyoendesha programu zake katika jitihada za kuendeleza sekta ya michezo nchini.
“Nawapongeza viongozi, wafanyakazi na wanachuo kwa juhudi mnazofanya katika
kukiimarisha chuo hiki ambacho ni hazina ya michezo mbalimbali nchini, mmepiga
hatua kubwa ya kimaendeleo” alisema Prof. Ole Gabriel.
Chuo hicho kimekuwa msingi wa kujenga wataalam wa michezo nchini kwa lengo la
kuimarisha mahusiano na maendeleo ya kielimu kijamii, kielimu, kikazi na kiuchumi
kwa kuzishirikisha halmashauri zote nchini.
Katika kuenedeleza michezo nchini, Prof. Ole Gabriel amewaambia viongozi wa chuo
hicho kuwa wawe wabunifu kwa kuongeza programu nyingi zaidi chuoni hapo ambazo
zitaongeza kipato na tija kwa chuo, wanachuo, wananchi wanazunguka chuo na taifa
kwa ujumla.
Aidha, Prof. Ole Gabriel ameongeza kuwa ni vema chuo hicho wapange na kuanzisha
mafunzo ya muda mfupi ili kurahisishs watu kupata elimu ya michezo na kuongeza tija
katika utendaji kazi.
Kwa upande wake Mkuu wa chuo Richard Mganga akitoa taarifa yake kwa Katibu Mkuu
mwenye dhamana ya michezo Prof. Ole Gabriel alisema kuwa chuo hicho kimepata
Ithibati kamili mwaka 2015 na kinafundisha kozi ambazo zinafuata mitaala
iliyopitishwa na Baraza la Taifa La Elimu ya Ufundi (NACTE).
Mkuu huyo aliongeza kuwa kwa mara ya kwanza chuo kimekuwa na wanafunzi wa
mwaka wa kwanza na wa pili kwa kozi za Stashahada ya Utawala na Uongozi katika
Michezo, Stashahada ya Elimu ya Michezo, Stashahada ya Ukocha tofauti na miaka ya
nyuma ambapo kulikuwa na wanafunzi mwaka moja tu.
Hali hiyo imefanya idadi ya wanachuo mwaka huu wa masomo 2016/2017 kuongezeka
ambapo hadi sasa wapo wanachuo 99 ambapo mwaka wa kwanza idadi yao ni 46 na
mwaka wa pili wakiwa 53.
Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Prof. Elisante Ole
Gabriel (wa pili kushoto) akiwasili Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya kilichopo
mkoani Mwanza wakati wa ziara ya kikazi mwishoni wa wiki kujionea namna chuo
hicho kinavyoendesha programu zake katika jitihada za kuendeleza sekta ya michezo
nchini. Wa kwanza kulia ni Mkuu wa chuo Richard Mganga na wa kwanza kulia ni Rais
wa Serikali ya wananchuo Cletus Mutakyawa.
Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Prof. Elisante Ole
Gabriel (wa nne kushoto aliyekaa) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi na
wanafunzi wa Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya kilichopo mkoani Mwanza wakati
wa ziara ya kikazi mwishoni wa wiki kujionea namna chuo hicho kinavyoendesha
programu zake katika jitihada za kuendeleza sekta ya michezo nchini.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...