Katika kuhakikisha kero ya Maji inakwisha kwenye maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam, Shirika la Majisafi na
Majitaka jijini Dar es salaam (DAWASCO) limezindua vizimba 8 vya Majisafi katika mtaa wa Mvuleni uliopo katika
kata ya Manzese wilaya ya Kinondoni, ili kuwapunguzia wakazi wa maeneo hayo adhaa ya kutafuta Majisafi na
salama kutoka umbali mrefu baada ya kuyakosa kwa takribani miaka 30.
Akizungumza katika uzinduzi huo wa vizimba vya Majisafi, Meneja wa Dawasco mkoa wa Magomeni, Mhandisi
Pascal Fumbuka, ameeleza kuwa wameamua kufikisha huduma ya Majisafi katika mtaa huo wa Mvuleni kwa njia ya
kujenga vizimba vya Majisafi kutokana na eneo hilo kutoingilika kimtaa, hivyo kupelekea kushindwa kuweka
mabomba ya Majisafi ya nyumba kwa nyumba.
Aidha, Mhandisi Fumbuka ameongeza kuwa, wapo kwenye jitihada za kuongeza mradi mdogo wa bomba la inchi 6
ambalo litasaidia kuongeza msukumo wa Majisafi ili kuwahudumia wakazi wengi zaidi wa maeneo hayo ya Mvuleni
pamoja na mitaa jirani ya Muungano na Kilimani.
“Katika kutatua kero ya Maji hapa Manzese Mvuleni, tumejenga vizimba vya Majisafi nane na tunatarajia wakazi
zaidi ya elfu thelathini na sita watanunufaika na vizimba hivi. Tumeshindwa kufikisha bomba kwa kila mkazi kutokana
na ujenzi holela wa makazi ya watu, lakini tuamini kuwa vizimba hivi vitasaidia kuondoa kero ya Maji kutokana na
msukumo wake wa Maji kuwa mkubwa, hivyo tunaamini havitaleta msongamano pamoja usumbufu kwa wakazi pale
watakapokuwa wanakinga Maji” alisema Mhandisi Fumbuka.
Kwa upande wa mwenyekiti wa serikali ya mtaa wa Mvuleni Bw. Mrita Mzee ameishukuru Dawasco kwa kujenga
vizimba hivyo vya Majisafi kwani wakazi wa mtaa wake walikuwa wakipata adhaa ya kutafuta Majisafi na salama
kutoka umbali mrefu na kwa muda mrefu, amewataka wananchi kuvitunza pamoja na kuvilinda vizimba hivyo vya
Majisafi ili viweze kuwasaidia kwa kipindi kirefu zaidi.
“Nawashukuru sana Dawasco Magomeni na uongozi wake kwa kutukumbuka na kujengea vizimba hivi vya Majisafi,
naamini vitaondoa kero ya Maji iliyokuwepo awali na niwaombe tu wananchi kushirikiana kwa pamoja katika
kuvitunza na kuvilinda vizimba hivi ili kuepuka kurudi tena katika shida ya Maji tuliyokuwa nayo hapo awali” alisema
Bw. Mzee.
Naye, mkazi wa mtaa huo wa Mvuleni Bi. Hawa Mohamed amesema kuwa vizimba hivyo vya Majisafi vimekuwa
mkombozi mkubwa kwao kwani wanawake ndio ambao wamekuwa wakihangaika kutafuta Majisafi kwa muda mrefu,
hivyo kusababisha kushindwa kufanya shughuli zingine za kimaendeleo. Aidha, ameiomba Dawasco kuongeza
vizimba katika sehemu iliyobaki ya mtaa huo ili kuepuka msongamano kwenye vizimba hivyo.
“Vizimba hivi vya Majisafi kwa kweli vimetuokoa sisi wanawake wa mtaa wa Mvuleni maana tulikuwa tunapata shida
mno kuyapata na tulikuwa tukiyanunua kwa bei ya juu sana, bei ambayo sisi watu wakawaida ilikuwa inatuwia
vigumu kuimudu” alisema Bi. Hawa.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...