Na  Bashir  Yakub. 
Ni  wangapi  wamefanyiwa  utapeli  katika  harakati  za  kununua  viwanja  au  nyumba.  Ni  wangapi  wamepata  hasara  kubwa  kutokana  na  michezo  ya  utapeli   iliyotamalaki  katika  ardhi  nchini.  Ni  kesi  ngapi  ziko  mahakamani  zinazohusisha  utapeli   katika  mauzo na  manunuzi  ya  ardhi.  Idadi  ni kubwa  mno  na huu  ndio  ukweli.

Siku  zote  huwa tunasema  ni  vigumu  kujua   ukubwa  na  hatari  ya  jambo   hili  mpaka  likukute  au  limkute  mtu  wako  wa  karibu. Lakini  swali  ni  ikiwa  watu   wamekuwa  wakijifunza  kupitia  wenzao  ambao  wamekutwa  na  haya. Kama  na wewe  bado  hujajifunza  basi ni  muhimu  sasa  kujifunza.

Mtu   anauza  ardhi  moja  kwa  watu hata   zaidi  ya  wanne tofauti, mtu  anauza  ardhi  asiyokuwa  yake  huku  akijua  kabisa  sio  ya kwake, mtu  anaghushi  hati  au  leseni  ya  makazi  kisha  anauza  kiwanja  au  nyumba ya  mtu, kiongozi  wa  serikali  ya  mtaa   anashiriki  kuuza  ardhi  ya mtu   huku akijua  kuwa  juzi  mtu  mwingine  alinunua  ardhi  hiyohiyo, kwa  ufupi  hali  ni  mbaya  na  ni  vema  kusema  ili  watu  wachukue  tahadhari.

Wizara  ya  ardhi  imeshasema mara  nyingi  kuwa  moja  ya  sababu  kubwa  inayopelekea  watu   kutapeliwa  katika  manunuzi  ya  ardhi  ni  wanunuzi  wenyewe  kutozingatia  taratibu  za  kisheria  za  manunuzi. Migogoro  mingi  imezalika  hapa. 

Mara  kadhaa  tumewahi  kueleza  kwenye  makala mbalimbali  namna  salama  ya  kununua  ardhi  kwa  kuepuka  utapeli.  Zipo  makala nyingi  ambazo  zimeeleza  hatua  za  kufuata  ili  uwe  salama.  Hata  hivyo  leo  kitaelezwa  kitu  kingine  ambacho  hakikuwahi  kuelezwa.  Ni  namna  ya kuhakiki  hati  au  leseni  ya  makazi   ili  kujua  ikiwa ni  halisi (original)  au  feki kabla  ya  kununua  kiwanja  au  nyumba. 

1.UHAKIKI  ULIOWAHI  KUSHAURIWA.
Kabla  ya  kueleza  njia  nyingine  ya uhakiki  inayotakiwa  kuelezwa  leo hebu  tujikumbushe  njia iliyowahi  kuelezwa  katika  makala  zilizopita. Ni  uhakiki  wa  hati  kwa  njia  ya   upekuzi  rasmi( official  search).  Tulisema  kuwa  kupitia  njia  hii  utaandaa  maombi  kwenda  kwa   msajili  wa  hati(Registrar of Title)   ukitaka  kujua  ikiwa  nyumba /kiwaja  unachotaka  kununua  kama kina  mgogoro  au  ikiwa kuna  mtu  mwingine  mwenye  maslahi  juu  yake.

Mgogoro  ni  kama  kuna  zuio  la  kifamilia( caveat), zuio  kutoka  mahakamani  na  mengine  yanayofanana  na  hayo.  Na  kuwapo  mtu  mwingine  mwenye  maslahi  ni  kama  kiwanja  au  nyumba hiyo kuwa   imesimama  kama  dhamana   ya  mkopo n.k.  Majibu  ya  vitu  vyote  hivi  utayapata utakapojibiwa   maombi  yako  ya  upekuzi  rasmi ( official  search).

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...