Na Mwandishi Wetu, TPA
Waziri
Mkuu wa Shirikisho la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ethiopia, Mhe. Hailemariam
Desalegn amesema Shirika la Meli la Ethiopia (Ethiopian Shipping Line) lipo
tayari kuanza kuitumia Bandari ya Dar es Salaam kutokana na kutoa huduma nzuri.
“Shirika letu la Meli ambalo ni
la kihistoria na lililobaki pekee katika ukanda wa Afrika likiwa linamilikiwa
na Serikali ya Ethiopia sasa lipo tayari kufanya kazi na Mamlaka ya Usimamizi
wa Bandari Tanzania,” amebainisha Mhe. Desalegn.
Ameongeza kuwa mbali na shirika
hilo la meli kuwa tayari kuanza kuleta meli zake Bandari ya Dar es Salaam pia
Shirika Kongwe la Ndege la Ethiopia (Ethiopian Airline) lenye mafanikio makubwa
nalo litaanza kusafirisha mizigo inayopitishwa katika Bandari ya Dar es Salaam.
Kwa upande mwingine Mhe.
Desalegn amepongeza jitihada kubwa zinazofanywa na Menejimenti ya TPA katika
kuboresha huduma zake ambapo amesema jitihada hizo sio tu zitanufaisha Serikali
zote mbili bali pia ustawi wa maisha ya watu wa Tanzania na Ethiopia nao
utaimarika.
Kwa upande wake Waziri Mkuu wa
Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Kassim amemshukuru Waziri Mkuu wa Ethiopia kwa
kuja nchini ambapo amemuahidi kwamba mahusiano mazuri yaliyopo baina ya nchi
hizi mbili yatadumishwa kwa maslahi mapana ya mataifa yote.
Awali akimkaribisha Waziri Mkuu
wa Tanzania, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Makame Mbarawa
amesema TPA itaendelea na mipango iliyopo ya kuhakikisha inaboresha Bandari zake
ili ziweze kuhudumia vyema wateja wote kwa wakati.
“Tutaendelea kuboresha huduma
zetu za Bandari na za sekta ya uchukuzi kwa ujumla ili tuweze kufikia malengo
yenu na wateja wetu ya kuhakikisha kwamba tunawahudumia vizuri na kwa ufanisi,”
amesema Mhe. Mbarawa.
Mapema akitoa taarifa ya
utendaji wa Mamlaka, Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Mhandisi Deusdedit Kakoko
alimweleza Waziri Mkuu wa Ethiopia kwamba kwa sasa TPA inaendelea na mpango
wake wa kujenga uwezo wa kuhudumia wateja wake kwa kuzingatia kwamba sekta ya
uchukuzi inakuwa kwa kasi.
“Kutokana na kasi kubwa ya
ukuaji wa uchumi nchini na Duniani kwa ujumla, TPA inaimarisha uwezo wake wa
kuhudumia mizigo na meli kubwa ili kujenga uwezo kabla ya mahitaji makubwa
kujitokeza”, amesisitiza Mhandisi Kakoko.
Waziri
Mkuu wa Shirikisho la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ethiopia, Mhe. Hailemariam
Desalegn (katikati) akifurahia zawadi ya picha ya Bandari ya Dar es Salaam mara
baada ya kukabidhiwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TPA, Pro f. Ignas Rubaratuka
(kulia). Kushoto ni Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim
Majaliwa Kassim.
Waziri
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Kassim
akisalimiana na Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya TPA mara baada ya kuwasili
bandari ya Dar es Salaam kumpokea mgeni wake Waziri Mkuu wa Shirikisho la
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ethiopia, Mhe. Hailemariam Desalegn hivi karibuni.
Mkurugenzi
Mkuu wa TPA, Mhandisi Deusdedit Kakoko akisalimiana na Waziri Mkuu wa Shirikisho
la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ethiopia, Mhe. Hailemariam Desalegn mara baada ya
kuwasili bandari ya Dar es Salaam hivi karibuni kwa ziara fupi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...