WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemsimamisha kazi Mkurugenzi Msaidizi wa Pembejeo wa Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Bw. Shenal Nyoni ili kupisha uchunguzi wa tuhuma zinazomkabili kwa kuongeza gharama za pembejeo kwa kushirikiana na baadhi ya mawakala wa pembejeo za kilimo.
Amesema
Serikali italipa madeni yote ya mawakala wa pembejeo za kilimo mara baada ya kukamilisha
uhakiki na kujiridhisha juu ya uhalali wake, sababu bado inawahitaji mawakala
ili kushirikiana nao katika kuhudumia wakulima kwenye maeneo mbalimbali nchini.
Waziri Mkuu
ametoa kauli hiyo leo (Jumatatu, Aprili 10, 2017) katika kikao alichokiitisha
kwenye Makazi ya Waziri Mkuu mjini Dodoma kati yake na mawakala wa pembejeo za
kilimo pamona na Maofisa kutoka Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.
“Gharama ya
madeni ni kubwa kuliko pembejeo zilizosambazwa. Hii inatokana na udanganyifu
mkubwa unaofanywa na mawakala kwa kushirikiana na watendaji wa Serikali wanaohusika
na masuala ya pembejeo,”
Amesema kuwa
kwenye eneo la pembejeo kuna matatizo makubwa kutokana na baadhi ya Maofisa kuzungumza
na mawakala na kuongeza gharama za pembejeo kwa lengo la kuibia Serikali na kisha
kugawana fedha. “Sasa Serikali haiwezi kulipa madeni ya kutengenezwa bali
tutawalipa stahili zenu baada ya uhakiki kukamilika kama nilivyosema awali,”.
Waziri Mkuu
ameongeza mawakala wa pembejeo waliwasilisha Serikali deni la sh. bilioni 65.4
kwa huduma waliyoitoa katika mikoa 25 ambapo Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi
imekamilisha uhakiki wa madeni hayo kwa mikoa 10 ya Morogoro, Iringa, Njombe,
Ruvuma, Songwe, Rukwa, Katavi, Kigoma, Kilimanjaro na Arusha ambayo madeni yake
ni asilimia 70 ya madeni yote.
Amesema ripoti
ya uhakiki wa mikoa nane kati ya 10 imetoka (imebaki Katavi na Kigoma) na
kubainisha kuwa mikoa hiyo inadai sh. bilioni 36 kati ya hizo sh. bilioni 11
bado zinaendelea kuhakikiwa, sh. bilioni 14 zimekataliwa hivyo siyo madeni
halali, sh. bilioni 8.2 ndiyo deni halali na sh. bilioni 2.3 zinachungizwa na Taasisi
ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).
Waziri Mkuu amesema
uhakiki wa madeni kwa mikoa 15 iliyobakia ambayo madeni yake ni asilimia 30
unaendelea ambapo amewasihi mawakala hao kuwa wavumilivu katika kipindi ambacho
Serikali inafanya uhakiki kwa kuwa inataka itende haki kwa kila mtu kulipwa
deni lake kwa kiwango kinachostahili na watakaobainika kufanya udanganyifu
watachukuliwa hatua za kisheria.
IMETOLEWA
NA:
OFISI
YA WAZIRI MKUU,
S.L.P
980, DODOMA
JUMATATU,
APRILI 10, 2017.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...