Serikali
ya Marekani kupitia Mpango wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kukabiliana na
UKIMWI (PEPFAR), umeidhinisha mpango wa kutoa Dola za Kimarekani Milioni 526
katika kipindi cha mwaka mmoja ujao kwa ajili ya kukabiliana na VVU/UKIMWI
nchini Tanzania. Msaada huu utaongeza idadi ya Watanzania wanaopatiwa matibabu
ya kufubaza VVU kufikia milioni 1.2 na utaimarisha mapambano dhidi ya VVU
kupitia huduma za upimaji, matibabu, kufubaza (viral suppression) na kuzuia
maambukizi ili hatimaye kufikia lengo la kuutokomeza kabisa UKIMWI ifikapo
mwaka 2030.
Fedha
hizo zitafadhili miradi mbalimbali inayotekelezwa chini Mpango wa Utekelezaji
wa PEPFAR Nchini utakaoanza kutekelezwa
Mwezi Oktoba 2017 hadi Septemba 2018, na ni ongezeko la asilimia 12.3 ya bajeti
ya mwaka jana. Chini ya mpango huu mpya,
PEPFAR itafanya kazi na Serikali ya Tanzania na wabia wake kadhaa kutoa huduma
ya upimaji wa VVU kwa Watanzania milioni 8.6 na kutoa matibabu ya kufubaza VVU
kwa watu 360,000 watakaobainika kuwa wameambukizwa virusi hivyo kufanya idadi
ya Watanzania watakaokuwa wakipata matibabu hayo kufikia milioni 1.2. Bajeti iliyotengwa inajumuisha pia utoaji wa
huduma na matibabu kwa watoto yatima na wale walio katika mazingira hatarishi
pamoja na kukabiliana na ukatili wa kijinsia.
Hali kadhalika, katika kuimarisha jitihada za kuzuia maambukizi mapya ya
VVU, PEPFAR itasaidia mpango wa tohara ya hiari kwa wanaume (VMMC) ambapo
wanaume 890,000 watapatiwa huduma hiyo.
Mpango huu unaendeleza ubia wa muda
mrefu kati ya Marekani na Tanzania katika sekta ya afya ikiwa ni pamoja na
muongo mmoja wa ushirikiano uliowezesha kudhibiti kwa mafanikio makubwa
maambukizi ya VVU na kufanyakazi tukilenga katika kuwa na Kizazi kisicho na
UKIMWI. Akitoa maoni yake kuhusu mpango huu ulioidhinishwa, Kaimu Balozi
wa Marekani nchini Virginia Blaser alisema “Kwa niaba ya Watu wa Marekani tuna
furaha kubwa kuendelea kuwasaidia watu wa Tanzania na kuendeleza ubia uliopo
baina yetu. Kwa pamoja tunafanya kazi ili hatimaye kuwa na Kizazi Kisicho na
UKIMWI Tanzania – ambacho hakuna hata mtu mmoja anayeachwa nyuma.”
Wadau
na wabia wa PEPFAR walioshiriki katika uandaaji wa mpango huu na watakaoshiriki
katika utekelezaji wake ni pamoja na Wizara ya Afya, Ustawi wa Jamii, Jinsia,
Wazee na Watoto, Tume ya Taifa ya Kudhibiti UKIMWI (TACAIDS), Programu ya
Pamoja ya Umoja wa Mataifa ya Kudhibiti VVU/UKIMWI (UNAIDS), Mfuko wa Kimataifa
wa Kupambana na Kifua Kikuu, UKIMWI na Malaria (GFTAM), Shirika la Afya Duniani
(WHO), Taasisi ya Bill na Melinda Gates, Taasisi ya Benjamin Mkapa ya
kukabiliana na VVU/UKIMWI (BMAF) na Mtandao wa Kitaifa wa Wanawake wanaoishi na
VVU/UKIMWI (NETWO+).
Kwa
taarifa zaidi kuhusu PEPFAR nchini Tanzania tafadhali tembelea tovuti ya
Ubalozi wa Marekani https://tz.usembassy.gov/our-relationship/pepfar/.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...