Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Bw. Kailima Ramadhani
(kulia) akifafanua jambo wakati akitoa elimu ya mpiga kura kwenye kituo cha
redio Dodoma FM cha mjini Dodoma.Kulia kwake ni Afisa wa Tume Bw. Mawazo
Bikenye na mbeye ni watangazaji .Picha na Hussein Makame, NEC-Dodoma.
Hussein Makame-NEC, Dodoma
Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeanza maandalizi ya kufanya uboreshaji
wa daftari la kudumu la wapiga kura kwa mwaka wa fedha wa
2017/2018 baada ya Serikali kutenga Shilingi Bilioni 10 kwa ajili ya kazi
hiyo katika bajeti ya mwaka ujao wa fedha.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Tume hiyo Bw. Kailima
Ramadhani kwa nyakati tofauti wakati akitoa elimu ya mpiga kura
katika vituo vya redio vilivyoko mkoani Dodoma.
Alisema kuwa maandalizi ya uboreshaji huo ni pamoja na kutoa elimu
ya mpiga kura kupitia vituo vya redio nchi nzima mpango ambao
umeanza kutekelezwa kwa baadhi ya mikoa nchini.
“Tume imeanza maandalizi ya kufanya uboreshaji wa daftari la kudumu
la wapiga kura, Serikali imeshatenga Shilingi Bilioni 10 kwa ajili ya
kuboresha daftari la kudumu la wapiga kura mwaka 2017/2018”alisema
Bw. Kailima.
Aliongeza kuwa kwa kipindi hicho Tume itatoa kadi mpya ya mpiga kura
kwa watakaoandikishwa upya, waliopoteza kadi na kadi zilizoharribika,
kwa wanaohamisha taarifa zao ikiwemo waliohamia Dodoma, na kufuta
wapiga kura waliopoteza sifa za kuwa wapiga kura.
Bw. Kailima aliwataka wananchi wafuatilie elimu ya mpiga kura
inayotolewa kupitia redio ya mikoani kuelewa mambo mbalimbali
yanayohusu mchakato wa uchaguzi ili fikapo mwaka 2020 kila
mwananchi awe ameelimika na asiweze kupotoshwa.
Alisema kwamba kwa muda mrefu elimu ya mpiga kura imekuwa
haitolewa kwa mujibu wa matakwa ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania na Sheria ya Taifa ya Uchaguzi.
Alifafanua kuwa Ibara 74 (6) (e) ya Katiba inaitaka Tume kutekeleza
majukumu kwa mujibu wa Sheria nyingine yiyite iliyotungwa na Bunge
na Ibara ya 18 inampa kila mwananchi haki ya kupata taarifa muhimu
zinazohusu nchi yake
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...