Aliyekuwa Katibu Mkuu, Wizara ya Ardhi, Nyumba na
Maendeleo ya Makazi; Dkt. Yamungu Kayandabila amesisitiza utumishi bora
unaozingatia Miongozo na Sheria.
Dkt. Kayandabila aliyeteuliwa hivi karibuni na Mhe. Rais,
Dkt. John Pombe Magufuli kuwa Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), akiwaaga
Watumishi wa Wizara alihimiza utendaji bora kazini katika kutoa huduma kwa
Wananchi na kusihi Watumishi kuendelea na kasi hiyo.
Aidha, aliwashukuru Watumishi wa Wizara ya Ardhi kwa
ushirikiano wao walioonyesha kwake ambao umesababisha kudhihirisha matukio
chanya kwa Wizara. Alisema; “ Tukumbuke kuwa sisi ni Watumishi wa Umma,
tuendelee kufanya kazi kwa bidii kwa kuwahudumia Wananchi kwa bidii”.
Awali akizungumza kwa niaba ya Watumishi wa Wizara; Afisa
Mipango Miji, Baltazar Sumari alisema; “ Tunakushukuru Katibu Mkuu kwa jinsi
ulivyotuwezesha kufanya kazi kwa umoja na nidhamu, Mungu akuwezeshe uweze
kuendelea kudumisha utendaji wako wa kazi Benki Kuu kama jinsi ulivyofanya
Wizarani hapa na tutaendelea kuhitaji ushauri wako”.
Naye muwakilishi wa Taasisi za Wizara; Msajili wa Bodi ya
Usajili wa Wataalamu wa Mipangomiji (TPRB);
Helena Mtutwa alisema kuwa Dkt. Kayandabila ana karama ya kipekee ambayo
imemuwezesha kuongoza vyema kwa kuweza kuonyesha njia bora katika utendaji kazi
na kuonya kwa hekima.
Dkt. Kayandabila anakwenda kutumika katika Benki Kuu ya
Tanzania kama Naibu Gavana anayeshughulikia Uchumi na Fedha (Economic
and Financial Policies – EFP), akiwa na Naibu Gavana mwenza
aliyeteuliwa naye kwa kipindi kimoja; Dkt. Bernard Yohana Kibese atakayehusika
katika eneo la Uthabiti na Usimamizi wa Sekta ya Fedha (Financil Stability and Deepening
– FSD).
Na kitengo cha Mawasiliano
Serikalini –
Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
Aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Nyumba na
Maendeleo ya Makazi Dkt. Yamungu Kayandabila akizungumza na watumishi alipokua
akiwaaga. Dkt. Kayandabila ameteuliwa na Mhe. Rais kuwa Naibu Gavana wa Benki
Kuu ya Tanzania. (BoT).
Aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Nyumba na
Maendeleo ya Makazi Dkt. Yamungu Kayandabila akipokea zawadi, ikiwa ni ishara
ya pongezi kwa uteuzi wake mpya alioupata. Anayemkabidhi zawadi hiyo kwa niaba
ya watumishi wa wizara ni Naibu Katibu Mkuu, Dkt Mosses Kusiluka.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...