Frank Mvungi-Maelezo
Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali imedhamiria  kuimarisha Ofisi za Kanda ili kusogeza huduma kwa wananchi katika Mikoa yote, ikiwa ni katika juhudi zake za kuimarisha utendaji na kuongeza tija na uwajibikaji.

Kauli hiyo imetolewa  leo Jijini Dar es Salaam na Meneja Mawasiliano na Masoko wa Ofisi hiyo Bw. Cletus Mnzava ,alipozungumza na waandishi wa  habari juu ya   majukumu ya Ofisi hiyo na huduma zinazotolewa.

“Mwelekeo ni kuimarisha Ofisi zetu za Kanda ili kusogeza huduma karibu  kwa wananchi, kwa sasa tunaendelea kuimarisha Ofisi ya Dodoma kama Makao Makuu ya Nchi ambayo pia itahudumia Mikoa ya Iringa,Morogoro na Singida” Alisisitiza Mnzava.

Akifafanua Mnzava alisema Ofisi hiyo imejipanga kuendana na sera ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kujenga Tanzania ya Viwanda  kwa sababu viwanda vitakuwepo kila kona ya nchi na viwanda vinatumia kemikali hivyo vinatakiwa vifuatiliwe kwa ukaribu ili matumizi yafanyike kwa mujibu wa Sheria na taratibu zilizowekwa.

Aliongeza kuwa moja ya mikakati ya Ofisi hiyo ni kuwepo kwa watumishi wanaodhibiti uingizwaji wa kemikali usiofuata taratibu ambapo wakaguzi hao kwa sasa wako katika mipaka ya Namanga,Holili na Horohoro kwa upande wa kanda ya Kaskazini.

Kwa upande wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini wakaguzi hao wako katika mipaka ya Tunduma,Kasumulu na Mutukula ,Sirari kwa upande wa Kanda ya Ziwa ambapo mpango mkakati wa Ofisi hiyo ni kuhakikisha kuwa Lengo la Serikali kusogeza huduma karibu na wananchi linatimia.

Kwa upande wake Meneja wa Ukaguzi wa Kemikali Bw. Fidelis Segumba amesema Maabara hiyo imejipanga kuwahudumia wananchi vizuri nyakati zote.
Meneja Mawasiliano na Masoko wa kutoka Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali Bw. Cletus Mnzava akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam kuhusu uimarishaji wa Ofisi za Kanda ili kusogeza huduma karibu na wananchi. Kushoto ni Afisa Habari wa Ofisi hiyo Bw. Sylivesta Omari.
Meneja ukaguzi wa Kemikali Bw. Fidelis Segumba akisisitiza jambo kwa waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam.kulia ni Meneja Mawasiliano na Masoko wa Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali Bw. Cletus Mnzava (Picha na Frank Mvungi-Maelezo)

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...