MBUNGE wa Viti Maalumu Mkoa wa Iringa, Rose Tweve (CCM) amepanga kutumia zaidi ya Sh Milioni 60 kutoka katika mshahara wake kuwawezesha wanawake katika kata 107 za mkoa wa Iringa kuanzisha mifuko maalumu ya kuwezeshana kiuchumi.

Zaidi ya kata 40 za wilaya ya Iringa, Kilolo na Mufindi zimekwishanufaika na mpango huo unaokiwezesha kikundi cha wanawake katika kila kata kupata Sh 600,000 ambazo hazirudishwi. Akikabidhi kiasi hicho cha fedha kwa vikundi vya kata za Nyololo na Malangali, Tweve alisema zoezi hilo litaendelea katika kata zingine zote zilizobaki zitakazokamilisha taratibu mbalimbali ikiwemo ya kuunda uongozi wake na kufungua akaunti benki.
Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Iringa, Rose Tweve (CCM) akifurahi pamoja na wananchi wa kata ya Nyololo wakati wa muendelezo wa ziara yake kata 107 ya kuwahamisha wanawake wajiinue kiuchumi kwa kutumia vikundi pamoja na kuwawezesha kwa kuwapatia kiasi cha shilingi laki sita (600,000) kwa ajili ya kujiendeleza.

Tweve alisema kwa kupitia mifuko hiyo itakayojulikana kama mifuko ya Rose Tweve ya kila kata wanawake watajiwekea utaratibu wa kuweka na kukopa, kuinuana kimaendeleo na kubuni mambo mengine yatakayowazidishia kasi ya maendeleo yao. “Wanawake tupo wengi sana, lakini tunakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazoturudisha nyuma. Huu ndio muda wa kujipanga upya na kubadili maisha yetu kwa kutumia kauli mbiu ya rais wetu Dk John Magufuli ya Hapa Kazi tu,” alisema.

Alisema kutakuwepo na utaratibu wa kuvifanyia tathimini vikundi hivyo na vile vitakavyofanya vizuri vitapata nyongeza ya fedha kila mwaka kwa kupitia mpango huo na matokeo chanya yatakayojitokeza katika vikundi hivyo yatamshawishi atafute wafadhili wengine wa ndani na nje ili wasaidie zaidi.
Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Iringa, Rose Tweve (CCM) akizungumza na wananchi wa kata ya Nyololo wakati wa muendelezo wa ziara yake kata 107 ya kuwahamisha wanawake wajiinue kiuchumi kwa kutumia vikundi pamoja na kuwawezesha kwa kuwapatia kiasi cha shilingi laki sita (600,000) kwa ajili ya kujiendeleza.

“Nimeanzisha mpango huu kwa kutumia rasilimali zangu mwenyewe na kwangu mimi naona hili la kusaidia wanawake wenzangu kwa kutumia rasilimali zangu linawezekana, sitoi fedha hizi ili mgawane kwa matumizi yasiofaa, natoa kama jitihada zangu za kuwahamasisheni kuona haja ya kuwekeza kwa pamoja na kwa manufaa ya wote,” alisema.

Akishukuru kwa mchango huo, mmoja wa viongozi wa kikundi cha wanawake wa mfuko wa Rose Tweve wa kata ya Malangali, Judith Kisinini alisema wako katika mchakato wa kuanzisha duka la kuuza pembejeo za kilimo, hatua itakayowawezesha wanawake wakulima wa kata hiyo kupata huduma hiyo kwa gharama nafuu.
Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Iringa, Rose Tweve (CCM akikabidhiwa zawadi ya kitenge na wanawake wa kata ya Malangali Mkoa wa Iringa wakati wa muendelezo wa ziara yake kata 107 ya kuwahamisha wanawake wajiinue kiuchumi kwa kutumia vikundi pamoja na kuwawezesha kwa kuwapatia kiasi cha shilingi laki sita (600,000) kwa ajili ya kujiendeleza.

Kisinini alisema kikundi chao chenye wanachama zaidi ya 200 hadi sasa kimejiwekea taratibu mbalimbali za kufikia malengo yao na kila mwaka kila mwanachama atalazimika kuchangia sh 50,000 kama hisa. “Fedha hizo pamoja na michango ukiwemo wa mheshimiwa mbunge na faida tutakayokuwa tunapata kutoka katika shughuli tutakazokubaliana kufanya zitatumika kuendeleza wanachama wote bila ubaguzi wowote,” alisema.

Diwani wa kata ya Malangali ambaye pia ni katibu wa mbunge huyo, Shakila Salim aliunga mkono juhudi za mbunge huyo kwa kuvichangia vikundi hivyo Sh 100,000 kila kimoja na Tweve alikipongeza kikundi cha kata ya Mtitu wilayani Kilolo ambacho mapema mwaka huu alikipatia kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya kutunisha mfuko wake ambao sasa una zaidi ya Sh Milioni 1.8.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...