Benny Mwaipaja, WFM- Dar es Salaam.
SERIKALI imeipatia Benki ya
Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), shilingi 209.5 bilioni kwa ajili ya
kuendeleza Sekta ya Kilimo na Mifugo hapa nchini, leo, Jijini Dar es
salaam.
Akiongea kwa niaba ya Serikali
wakati wa tukio la utiaji saini mkataba wa makabidhiano ya fedha hizo,
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Khatibu Kazungu,
alisema kuwa kiasi hicho cha fedha ambacho ni mkopo wenye masharti nafuu
kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), ni sehemu ya shilingi 800
bilioni ambazo Serikali inatarajia kuipatia Benki hiyo ili iweze kukuza
mtaji wake.
“Ninaishukuru Benki ya Maendeleo
ya Afrika AfDB kwa kuipatia Serikali mkopo wa Dola za Marekani 93.5
milioni ambazo ni sawa na kiasi hicho cha fedha cha Sh. 209.5 bilioni
kwa ajili ya kuiongezea mtaji TADB ili iweze kuwafikia wakulima wengi
zaidi kwa kuwapatia mikopo yenye riba nafuu” alisema Dkt. Kazungu.
Alisema kuwa fedha hizo
zitasaidia kutatua changamoto ya upatikanaji wa mitaji kwa ajili ya
ujenzi wa miundombinu ya sekta ya kilimo na mifugo ili kuongeza
uzalishaji na tija katika kilimo ili sekta hiyo iweze kuchangia zaidi
katika ukuaji wa pato la Taifa kuliko ilivyo sasa.
“Mwaka jana kilimo ambacho
kinategemewa na idadi kubwa ya Watanzania kilichangia wastani wa
asilimia 29.1 ya Pato la Taifa lakini tunataka kupitia Benki hiyo Sekta
ya kilimo iiwezeshe nchi kukua kiuchumi kwa zaidi ya asilimia 7 hadi 10
katika kipindi kifupi kijacho” aliongeza Dkt. Kazungu.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Khatibu Kazungu akisaini mkataba wa kuipatia Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) fedha za kuiongezea mtaji kiasi cha shilingi bilioni 209.5. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo Bw. Francis Assenga, Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dar es Salaam
Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Sheria kutoka Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Eligius Mwankenja (kushoto), na Mchumi kutoka Wizara hiyo Bw. Said Nyenge (kulia) wakiwaelekeza Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Khatibu Kazungu na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TADB Bw. Francis Assenga, maeneo maalumu ya kutiwa saini kwenye Mkataba wenye thamani ya Sh. 209.5 bilioni utakaoiwezesha Benki hiyo kutoa mikopo ya muda wa kati na mrefu kwa riba nafuu kwa wakulima wadogo wadogo, Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dar es Salaam
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Khatibu Kazungu (kushoto) akibadilishana mkataba na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania-TADB, Bw. Francis Assenga mara baana ya kusainiwa mkataba wa kuiongezea mtaji Benki hiyo wenye thamani ya Sh. Bilioni 209.5 ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2016/2021, Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dar es Salaam.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Khatibu Kazungu wakionesha mkataba waliokwisha usaini kwa waandishi wa habari (hawamo pichani) na kushoto kwake ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Francis Assenga, Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dar es Salaam
Wajumbe waliohudhuria hafla ya utiaji saini mkataba wa kuiongezea mtaji Benki ya Kilimo wenye lengo la kuunganisha maboresho ya sekta ya kilimo na mpango wa mageuzi ya viwanda wenye thamani ya Sh. 209.5 bilioni, Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dar es Salaam.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...