Na Ramadhani Ali – Maelezo Zanzibar.

Mkuu wa Kitengo cha Lishe kutoka Wizara ya Afya Bi. Asha Hassan amesema Zanzibar bado ipo nyuma katika kiwango cha Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) cha kuwapatia matone ya Vitamn A watoto wenye umri kuanzia miaka miwili hadi miaka mitano.

Bi. Asha alieleza hayo katika mkutano na waandishi wa habari kuhusu zoezi la kuwapatia matone ya Vitamen A watoto wenye umri huo lililoanza tarehe 1 Juni ambalo linategemea kumalizika mwishoni mwa mwezi huu kwa awamu ya kwanza mwaka huu na awamu ya pili itafanyika mwezi Disemba.

Alisema Zanzibar hadi hivi sasa imefikia asilimia 82 katika  mpango huo wakati kiwango kilichowekwa na Shirika la Afya  Ulimwenguni ni asilimia 95.Alizitaja Wilaya tatu za Mkoa Mjini Magharibi ndizo zenye asilimia ndogo zaidi chini ya asilimia 70 wakati Wilaya ya Kati inaongoza kwa kuwa na zaidi ya asilimia 95.

Alisema Kitengo kimeanzisha utaratibu wa kuwafuata wazazi wanaoishi mbali na vituo vya afya ili kuwapatia watoto  matone ya Vitamin A lakini baadhi ya wazazi wamekuwa hawatoi mashirikiano.

Aliwasisitiza wazazi kufanya juhudi kuhakikisha watoto wao wanapata matone hayo kwa vile ni muhimu katika kuimarisha kinga ya mwili dhidi ya maambukizo ya maradhi ikiwemo kuharisha na kutoona vizuri.Afisa Kitengo cha Lishe Wilaya ya Mjini Fatma Ali Saidi alisema kumekuwa na dhana potofu  kwa wananchi hasa wanaoishi mjini kwamba watoto wao hawahitaji matone ya Vitamin A kwa vile wanakula vizuri lakini dhana hiyo sio sahihi.

Alisema utafiti uliofanywa na Kitengo hicho unaonyesha kwamba watoto  wenye hali nzuri ya Vitamin A  Zanzibar ni asilimia 12 na asilimia 88 iliyobaki wanaupungufu.Aliwatoa wasi wasi wazazi kuwa hata wale wachache wenye Vitamin A vya kutosha mwilini wanapopewa matone hayo hayana madhara yoyote na wanaweza kutumia. 

Washiriki wa mkutano huo walikishauri Kitengo cha Lishe kuongeza kutoa elimu kwa wazazi kwani baadhi yao bado hawajaelewa umuhimu wa matone ya Vitamin A na wengine wanadhani kuwa matone hayo ni sawa na chanjo jambo ambalo sio sahihi.                            
 Mkuu wa Kitengo cha Lishe kutoka Wizara ya Afya Asha Hassan akizungumza na waandishi wa habari kuhusu zoezi la kuwapatia matone ya Vitamin A watoto wenye umri wa miaka miwili hadi mitano katika mkutano uliofanyika ukumbi wa Malaria Mwanakwerekwe.
 Washiriki wa mkutano huo wakiwa katika kazi za vikundi kupanga mikakati ya kuihamasisha jamii kuitikia kampeni ya kuwapatia watoto matone ya Vitamin A katika ukumbi wa Malaria Mwanakwerekwe.
 Mwandishi wa habari wa Gazeti la Zanzibar Leo Nasra Manzi akiwasilisha kazi ya kukundi chake katika mkutano wa kuwaelimisha waandishi kuhusu matone ya Vitamin A katika ukumbi wa Malaria Mwanakwerekwe.
Picha na Makame Mshenga.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...