Na Greyson Mwase, Geita
Naibu  Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani, ametoa siku 13 kwa mameneja wote wa Shirika la Umeme  Tanzania (TANESCO) kuhakikisha wananchi wote waliolipa ada kwa ajili ya kuunganishiwa huduma ya umeme wanaunganishiwa mapema na kuondokana na adha ya kuwepo gizani.
Dkt. Kalemani alitoa agizo hilo katika kijiji cha Nyijundu wilayani Nyang’hwale mkoani Geita wakati akizindua Mradi Kabambe wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu kwa mkoa wa Geita pamoja na kumtambulisha mkandarasi atakayetekeleza mradi kwa mkoa huo.
Alisema kuwa, ni haki ya mwananchi  aliyelipia gharama za kuunganishiwa umeme kupatiwa huduma ndani  ya siku saba kama sheria inavyofafanua na kuwataka mameneja kuhakikisha wananchi wote waliokuwa wamelipia huduma za kuunganishiwa  umeme kupata huduma hiyo kabla ya  Julai 25, mwaka huu.
Katika hatua nyingine, Dkt. Kalemani aliwataka mameneja  wa TANESCO  kusogeza huduma karibu na wananchi badala ya wananchi kusafiri  umbali mrefu  kwa gharama kubwa kufuata  huduma za umeme.
Alisema serikali ya awamu ya tano imedhamiria kuinua  uchumi wa viwanda kwa kuhakikisha nishati ya umeme ya uhakika inapatikana hususan katika maeneo ya vijijini ili wananchi waweze kujiajiri kupitia viwanda vidogo  vidogo kama mashine za kusaga na kukoboa nafaka, kuchomelea vyuma na kusindika matunda.
 Mkuu wa Mkoa wa Geita, Meja Jenerali Mstaafu Ezekiel Kyunga akielezea  hali ya upatikanaji wa umeme katika mkoa huo  mbele ya Naibu  Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani (hayupo pichani) kwenye uzinduzi huo.
 Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini na Mbunge wa Bukombe,  Dotto Biteko akifafanua jambo kwenye uzinduzi huo.
 Naibu  Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani akitoa maelekezo  kwa wakandarasi na watendaji kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) (hawapo pichani) kwenye uzinduzi huo.
 Sehemu ya wakandarasi na watendaji kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) wakipokea maelekezo kutoka kwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani (hayupo pichani) kwenye uzinduzi huo.
 Naibu  Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani akitoa sehemu ya  vifaa maalum vya Umeme Tayari (UMETA) kama zawadi kwa  sehemu ya wazee wa kijiji cha Nyijundu wilayani Nyang’hwale kwenye uzinduzi huo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...