Na Hyasinta Kissima, Njombe
Halmashauri ya Mji Njombe imerudisha heshima yake kwa kupata Hati safi katika ripoti ya mthibiti na mkaguzi wa serikali (CAG) kwa mwaka wa fedha 2015/2016) ambapo kwa mwaka wa fedha 2014/2015 Halmashauri hiyo ilipata hati inayoridhisha na yenye maswala ya msisitizo.
Akitoa mapendekezo yake wakati wa Mkutano Maalumu wa Baraza la Madiwani la kujadili hoja za Mthibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Katibu Tawala Mkoa wa Njombe  Jackson Saitabahu ameipongeza Halmashauri kwa kupata hati safi na kwa kukusanya mapato kwa asilimia 100.1 na amezitaka idara na vitengo vya Halmashauri kutoona Ofisi ya Ukaguzi wa ndani kama mwiba wa pori na mahali pasipoingilika kwani Kitengo hicho kipo kwa ajili ya kutoa ushauri lakini pia kuiandaa Halmashauri kwa Ukaguzi Mkuu hivyo wasisite kuomba ushauri pale inapobidi.
“Hati safi haiji kwa bahati mbaya, napenda niwapongeze kwa jitihada kubwa mlizoonyesha lakini pia niwasihi sana msikwepe Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani, Kitengo hiki kinatakiwa kiwezeshwe vizuri na Halmashauri ijenge mahusiano mazuri na Kitengo cha Ukaguzi kwani wakaguzi wa ndani ndio wanatuandaa kwa ajili ya ukaguzi wa nje.Tunapoimarisha mahusiano mazuri miongoni mwetu hatutakua na hoja za ukaguzi.Tusiwe mabingwa wa kujibu hoja zaidi ya kuwa wataalamu wa kuzuia hoja zisitokee.”Alisema Katibu Tawala.
Sambamba na hilo Halmashauri pia imeendelea kuimarika kwa kufikia asilimia 35% za kuweza kujitegemea jambo ambalo limeendelea kuifanya Halmashauri ya Mji Njombe kufanya vizuri katika shughuli mbalimbali za maendeleo.
Kwa mwaka 2017/2018 Halmashauri imejipanga kuhakikisha kuwa hoja zote zinafungwa, kukusanya mapato zaidi ya mwaka uliopita na kuhakikisha kuwa Halmashauri haitoruhusu kufanya biashara na Wakandarasi na wazabuni wasio na mashine za kielektroniki na kuhakikisha kuwa nyaraka na kumbukumbu zote za manunuzi zinatunzwa ipasavyo.
 Mweka Hazina wa Halmashauri ya Mji Njombe Dorcas Mkello akiwasilisha hoja za ukaguzi mbele ya Mkutano Maalumu wa  Baraza Kuu la Madiwani.
 Wakuu wa Idara na Vitengo Halmashauri ya Mji Njombe wakisikiliza kwa Makini mapendekezo ya Baraza la Madiwani.
 Katibu Tawala Mkoa wa Njombe Jackson Saitabahu akitoa mapendekezo yake mara baada ya kupitia hoja za ukaguzi.
Madiwani wakipitia makabrasha yenye hoja za Ukaguzi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...