MFUMUKO wa Bei wa Taifa kwa mwezi Juni, 2017 umepungua hadi asilimia 5.4 ikilinganishwa na asilimia 6.1 ilivyokuwa mwezi Mei, 2017.

Akizungumza na waandishi wa Habari leo jijini Dar es salaam, Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Takwimu za Jamii kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Ephraim Kwesigabo amesema Mfumuko wa Bei umepungua kutokana na kupungua kwa kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma kwa mwezi Juni, 2017 ikilinganishwa na kasi ya upandaji iliyokuwa kwa mwezi Mei, 2017.

“Mfumuko wa Bei wa mwezi Juni, 2017 umepungua hadi kufikia asilimia 5.4 kutoka asilimia 6.1 mwezi Mei, 2017. Hii inatokana na kupungua kwa kasi ya upandaji wa bei za bidhaa na huduma kwa mwezi Juni, 2017,” amesema Kwesigabo.

Amesema Mfumuko wa Bei unaopimwa kwa kipimo cha mwezi umepungua kwa asilimia 0.1 ikilinganishwa na ongezeko la asilimia 0.2 ilivyokuwa mwezi Mei, 2017.Kwesigabo amesema Fahirisi za Bei zimepungua hadi 109.10 mwezi Juni, 2017 kutoka 109.26 mwezi Mei, 2017. Amesema Kupungua kwa Fahirisi za Bei kumechangiwa hasa na kupungua kwa bei za baadhi ya bidhaa za vyakula.

Baadhi ya bidhaa za vyakula zilizochangia kupungua kwa fahirisi ni pamoja na mahindi ambayo yamepungua kwa asilimia 5.1, unga wa mahindi kwa asilimia 2.4, unga wa mihongo kwa asilimia 1.9, machungwa kwa asilimia 2.4, dagaa kwa asilimia 3.2, mbogamboga kwa asilimia 5.7, maharage kwa asilimia 1.8 na viazi mviringo kwa asilimia 6.2.

Aidha Mfumuko wa Bei kwa bidhaa za vyakula nyumbani na migahawani kwa mwezi Juni, 2017 umepungua hadi asilimia 9.8 kutoka asilimia 11.8 mwezi Mei, 2017.

Uwezo wa Shilingi 100 ya Tanzania katika kununua bidhaa na huduma umeimarika kidogo na kufikia Shilingi 91 na senti 66 mwezi Juni, 2017 ikilinganishwa na Shilingi 91 na senti 53 ilivyokuwa mwezi Mei, 2017.

Hata hivyo, Mfumuko wa Bei nchini Tanzania una mwelekeo unaofanana na baadhi ya nchi nyingine za Afrika Mashariki kwa kuwa Mfumuko wa Bei wa mwezi Juni, 2017 nchini Uganda umepungua hadi asilimia 6.4 kutoka asilimia 7.2 mwezi Mei, 2017; na nchini Kenya, Mfumuko wa Bei wa Mwezi Juni, 2017 umepungua hadi asilimia 9.21 kutoka asilimia 11.70 mwezi Mei, 2017.

Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Takwimu za Jamii Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Ephraim Kwesigwabo (kushoto), akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam leokuhusu mfumuko wa bei wa Taifa kwa Mwezi Juni. Kulia ni Meneja wa Takwimu za Bei na Ajira, Ruth Minja.
Mkutano na wanahabari ukiendelea.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...