Na Ramadhani Juma
Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI George Simbachawene ameahidi kumfikishia Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dokta John Magufuli ombi la kuitangaza
Manispaa ya Dodoma kuwa Jiji kwani inakidhi vigizo na kwamba sasa ni wakati
muafaka wa kupewa hadhi hiyo.
Alitoa ahadi hiyo jana
wakati akizungumza na watumishi wa Manispaa ya Dodoma katika Ukumbi wa Shule ya
Sekondari ya Dodoma ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya siku moja katika Manispaa hiyo,
iliyojumuisha pia ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo.
Aidha, amewataka watumishi
wa iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao (CDA) kumshukuru Rais kwa uamuzi wa
kuivunja Mamlaka hiyo kwa sababu hatua hiyo imeondoa mkanganyiko uliokuwepo
katika kuhudumia wananchi hususani katika sekta ya ardhi na mipango miji ambako
Manispaa ya Dodoma pia ilikuwa na jukumu hilo.
Pia aliwaeleza watumishi
hao wapatao 260 kuwa, sasa watapata fursa pana zaidi ya kuitumikia nchi yao
katika mikoa mbalimbali watakayopangiwa kuendelea kutumikia wananchi kwani wao
ni watumishi wa umma na wana haki na wajibu wa kufanya kazi sehemu yeyote
nchini.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI George Simbachawene (wa pili kushoto) akiingia katika Ofisi za Mhandisi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma kukagua magari na mitambo iliyorithiwa na Manispaa hiyo kutoka kwa iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA) wakati wa ziara ya siku moja ya Waziri huyo katika Manispaa hiyo jana. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Christine Mndeme na kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma Mhandisi Lusako Kilembe.
Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma Mhandisi Lusako Kilembe (kulia) akitoa maelezo kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI George Simbachawene wakati wa ziara ya siku moja ya Waziri huyo katika Manispaa hiyo. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Christine Mndeme. PICHA KWA HISANI YA BERN PATRICK WA GAZETI LA MWANANCHI.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...