Na
Thobias Robert- MAELEZO
Katibu Mkuu Jumuiya ya
Madola Mh. Patricia Scotland (picahni) anatarajiwa kufanya ziara ya kikazi ya siku tatu
hapa nchini, Katibu Mkuu wa Wizara ya mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika
Mashariki Balozi Dkt. Aziz Mlima amesema leo wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika
Kituo cha Mikutano cha kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es
Salaam.
Kwa mujibu wa Dkt.
Mlima. Katibu Mkuu huyo wa Jumuiya ya Madola
atafanya ziara ya siku tatu
nchini kuanzia Agosti 10 hadi 12 mwaka
huu, ambapo atakutana na viongozi wa juu wa serikali ya Tanzania.
“Lengo la ziara hiyo
nchini ni kuelezea viongozi wa ngazi za
juu wa Tanzania kuhusu mageuzi yanayofanywa na Sekrtarieti ya Jumuiya ya Madola
na vipaumbele vya Jumuiya hiyo kwa sasa, hatua zinazochukuliwa ili kuimarisha
kazi za Jumuiya hiyo na kutoa taarifa kuhusu Mkutano wa Wakuu wa Nchi na serikali wa Jumuiya
unaotarajiwa kufanyika jijini London
nchini Uingereza mwakani mwezi April” alisema
Dkt. Mlima.
Alifafanua kuwa mageuzi
yanayotarajiwa kufanywa na Jumuiya hiyo ni pamoja na kuondoa vyeo vya Naibu
Makatibu wakuu watatu na kupunguza idadi ya Wakurugenzi kutoka 12 hadi 6,
kuanzisha nafasi tano za Maafisa Waandamizi kutoka maeneo ya kijiografia ya
Jumuiya hiyo kwa maana ya Afrika, Ulaya, Amerika, Karibeani, Asia na Pacific
Kusini kwa lengo la kuziba nafasi ya Makatibu Wakuu.
“Mageuzi haya
yataiwezesha Jumuiya ya Madola kuokoa kiasi cha Pauni milioni 3 kwa mwaka
ambazo zitafanya kazi mbalimbali za kimaendeleo kwa nchi wanachama wa jumuiya
hiyo,” alifafanua Dkt. Mlima.
Katika ziara yake
nchini, Katibu Mkuu huyo wa Jumuiya ya Madola anatarajiwa kukutana na kufanya
mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe
Magufuli, Ikulu Jijini Dar es Salaam.
Mbali na kukutana na
Rais Magufuli, Katibu Mkuu Scotland atafanya mazungumzo na Waziri wa Elimu, Sayansi, na Teknolojia Prof.
Joyce Ndalichako pamoja na Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na
Mazingira Mhe. January Makamba.
Jumuiya ya Madola
ilianzishwa karne ya 20 kwa lengo la kuikutanisha Uingereza na yaliyokuwa
makoloni yake duniani kwa jukumu la kuhakikisha wanachama wanajikwamua katika nyanja za Kisiasa, Kiuchumi, kijamii,
Michezo na Burudani huku Malkia wa Uingereza ndiye Kiongozi Mkuu wa Jumuiya
hiyo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...