Shehena ya Rwanda kupitia bandari ya Dar es Salaam katika
kipindi cha miaka mitano imekuwa ikiongezeka kwa wastani wa
asilimia 9.9 kwa mwaka kutoka tani 630,000 mwaka 2012/2013
mpaka tani 950,000 mwaka 2016/2017.
Haya yamesemwa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya
Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) Mhandisi Deusdedit Kakoko
alipokutana na balozi wa Rwanda nchini Tanzania Mhe. Eugene
Kayihura aliyetembelea TPA leo.
Kakoko amesema kwamba kwa sasa shehena yote ya mizigo
inayokwenda na kutoka Rwanda na nchi zingine za jirani
inahudumiwa ndani ya bandari ili kurahisisha uondoshaji na
usalama wa mizigo hiyo.
Mkurugenzi Mkuu amesema katika mkakati wake wa kuimarisha
uhusiano zaidi na wateja, Serikali kupitia TPA imetenga eneo kwa
ajili ya kuhifadhia mzigo wa Rwanda katika bandari Kavu ya
Kwala, Ruvu na kuwataka wafanyabiashara wa nchini Rwanda
kuitumia bandari Kavu ya Isaka kwa ajili ya mizigo yao ili
kuwapunguzia safari ya kusafiri hadi Dar es Salaam.
TPA tayari imeshakamilisha ujenzi wa ofisi yake nchini Rwanda
kwa ajili ya kuhudumia wateja wake toka nchini humo. Kwa
mujibu wa Mkurugenzi Mkuu, ofisi hiyo ya TPA nchini Rwanda
imekamilika na kinachosubiriwa ni ufunguzi baada ya kukamilisha
taratibu zote ili ianze kazi rasmi.
“Ufunguzi wa ofisi hiyo utasaidia sana kuimarisha huduma kwa
wateja wetu wa Rwanda ambao wanatumia Bandari ya Dar es
Salaam,” amesema Kakoko.
Naye Balozi wa Rwanda nchini, Mhe. Eugene Kayihura
ameishukuru TPA na Serikali ya Tanzania kwa kuwapatia eneo la
kuhifadhia mizigo iendayo Rwanda.
Balozi Kayihura amesema kwamba biashara kati ya Tanzania na
Rwanda imekuwa ikiongezeka kwa kasi katika siku za hivi karibuni
mara baada ya TPA kuimarisha huduma zake.
“Kwa sasa Bandari ya Dar es Salaam imekuwa ikihudumia asimilia
90 ya mizigo yote inayoingia na kutoka Rwanda hivyo kuweka
rekodi ya ukuaji wa haraka sana wa mizigo ya Rwanda
inayohudumiwa nchini,” amesema Mhe. Balozi Kayihura.
Amesema kwamba ziara yake aliyoifanya bandarini ni sehemu ya
juhudi za Rwanda kuimarisha uhusiano wa kibiashara na Tanzania
haswa kwa kupitia huduma bora zitolewazo na Bandari ya Dar es
Salaam kwa sasa.
Katika mkakati wake wa kuhakikisha inakuwa karibu na wateja
wake, TPA hivi karibuni ilishiriki katika Maonesho ya Biashara ya
Kimataifa nchini Rwanda ambapo pamoja na mambo mengine
ilikutana na wafanyabiashara wa nchi hiyo ambao walionesha
kuridhishwa na huduma za bandari ya Dar es Salaam.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...