Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limeanza kutekeleza
shughuli za uwajibikaji kwa jamii katika mwaka wa fedha 2017/2018
ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali katika uboreshwaji
wa Sekta mbalimbali kama Elimu, Afya, Maji na Utawala Bora.
Hayo yamezungumzwa na Meneja wa Mawasiliano wa TPDC, Marie Msellemu katika tukio la kukabidhi hundi za fedha kwa ajili ya
kusaidia uimarishwaji wa Chama cha Maafisa Uhusiano Tanzania pamoja
na kukabidhi fedha za kuwezesha ununuzi wa mafuta na dawa kwa
Chama cha Wanawake Albino cha Ndugumbi lilofanyika tarehe 03
Novemba, 2017 Makao Makuu ya TPDC.
“Leo tunayo furaha ya kuanza rasmi shughuli zetu za uwajibikaji kwa
jamii kwa kuhakikisha afya bora kwa ndugu zetu kutoka kikundi cha
Wanawake Albino cha Ndugumbi kwa kuwapatia fedha za kuweza
kufanya manunuzi ya dawa na mafuta ya kupaka ili kuimarisha afya ya
ngozi zao na kujikinga dhidi ya maradhi ya Kansa na hivyo kurudisha
tabasmu kwao na kuona kuwa Shirika lao la Mafuta la taifa linawajali na
liko pamoja nao katika mapambano dhidi ya maradhi ya Kansa.” Msellemu alieza katika tukio hilo.
Meneja Mawasiliano wa TPDC akikabidhi hundi kwa Uongozi wa Chama cha Maafisa Uhusiano Tanzania.
Baada ya kupokea msaada wa fedha kutoka TPDC, Mwamvua Kambi
ambaye ni Katibu wa Ndugumbi ametoa shukrani kwa TPDC kwa
kuwajali na kuwasikiliza kilio chao maana kilio chao kikubwa ni Kansa ya
Ngozi ambayo kwa dawa na mafuta watakazonunua zitasaidia
kupunguza mionzi ya Jua ambayo ni hatarishi kwa afya za ngozi zao na
kwa msaada walioupata ni mkubwa na unawatosha pamoja na wenzao
katika kikundi.”
Aidha Meneja Mawasiliano alieongezea kuwa kwa kutambua umuhimu
wa kuboresha masuala ya Utawala Bora nchini, Shirika linaamini kuwa
kwa kukisaida Chama cha Maafisa Habari wa Tanzania kitakua kimeimarisha eneo la Utawala Bora ambapo kupitia Kongamano la
Maafisa habari ambalo litalenga kwenye kuimarisha mchango wao
katika kuijenga Tanzania ya Viwanda wataendelea kufanya kazi kwa
bidii kwa kuelimisha Umma wa Watanzania juu ya uwajibikaji wa
kizalendo katika kuiletea Nchi Yetu Maendeleo ya kweli katika Sekta ya
Viwanda.
David Mwaipaja ambaye ni Mratibu wa chama ametoa shukrani
kwa mchango wa TPDC, “Tunashukuru saana kwa utayari mliounyesha
wa kuhakikisha Chama cha Maafisa Uhusiano kinafikia Malengo yake na
kiukweli matokeo makubwa kwa mlichokifanya leo hayataonekana leo hii
lakini nafasi kubwa ya kushukuru itapatikana siku ya Mkutano
Utakaolenga kuangalia Nafasi ya Maafisa Uhusiano katika Kuelekea
Tanzania ya Viwanda ambapo mtapata nafasi ya kueleza umuhimu wenu
au mchango wenu katika kuijenga Tanzania ya Viwanda”.
Meneja Mawasiliano wa TPDC akikabidhi hundi kwa Chama Ndugumbi Albino kwa ajili ya kuwezesha manunuzi wa mafuta ya ngozi.
Msellemu anansisitiza kuwa “kwa Mwaka huu wa fedha TPDC
inatarajia kutekeleza ujenzi wa kituo cha Afya Tunduru, ujenzi wa vyoo
kwa wananfunzi wenye ulemavu Shule ya Msingi Shangani na vyoo kwa
Shule ya Msingi Kilwa Kivinje, ujenzi wa Zahanati katika kijiji cha Mingoji
pamoja na kufadhili zoezi la upimaji wa afya kupitia Taasisi ya Moyo
katika kuendesha zoezi la upimaji afya litakalofanyika Wilayani Luangwa
Mkoani Lindi.”
Msellemu amefafanua kuwa hii si mara ya kwanza kwa TPDC
kutekeleza jukumu lake la msingi katika uwajibikaji kwa jamii
inayoizunguka ila ni mwanzo tu wa shughuli hizo kwa mwaka huu wa
fedha.
“TPDC tumekuwa na utaratibu wa kutekeleza majukumu yetu kwa jamii
toka huko nyuma ambapo tuliweza kuchangia madawati na viti kwa
shule za Msingi na Sekondari kwa Mikoa ya Lindi, Mtwara na Dar es
Salaam, ujenzi wa madarasa, mabweni, vyoo, ofisi za serikali za mitaa
na n.k”.
TPDC kama Shirika la Mafuta la Taifa linao wajibu wa kutekeleza
majukumu yake kwa mujibu wa Sheria za Nchi na kama Sheria ya
Mafuta ya Mwaka 2015 inavyoelekeza namna ya utekelezaji wa wajibu
wa Sekta ya Mafuta na Gesi kwa jamii, Shirika litaendelea kutekeleza
wajibu huo kwa lengo la kuhakikisha manufaa ya Gesi Asilia nchini
yanapatikana kwa wananchi si kwa kutokana na mapato ya gesi asilia
pekee kwa Serikali lakini pia kwa kuboresha Sekta za Elimu, Afya, Maji,
Utawala Bora, Miundombinu na kadhalika.
Viongozi wa Chama cha Maafisa Uhusiano Tanzania na Chama cha
Ndugumbi pamoja na Meneja na Maafisa wa TPDC mara baada ya
makabidhiano ya Hundi katika Ofisi za TPDC Dar es Salaam.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...