Uwanja
wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam jana
ulikuwa eneo la majonzi makubwa baada ya miili ya askari 14 wa Jeshi la
Wananchi (JWTZ), waliouawa na waasi wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo
(DRC), kufika nchini hatimaye.
Miili
hiyo ilirejeshwa majira ya jioni na kupokelewa na umati wa askari wa
JWTZ wakiongozwa na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk.
Hussein Mwinyi pamoja na Mkuu wa Majeshi, Jenerali Venance Mabeyo.
Ni
mara ya kwanza kwa wanajeshi wengi kiasi hicho wa JWTZ kuuawa katika
misheni ya kulinda amani, kwa mujibu wa Jenerali Mabeyo aliyekuwa
akijibu maswali ya waandishi wa habari uwanjani hapo.
Miili hiyo ililetwa na ndege maalum ya Umoja wa Mataifa huku ikiwa imefunikwa bendera ya UN.
Baada ya kuwasili, kwa huzuni wanajeshi walianza kuchukua mwili mmoja baada ya mwingine na kuhamishia katika magari maalum yaliyokuwa yameandaliwa.
Kila mwili ulibebwa na wanajeshi nane wakati wa kuhamishia katika magari hayo kwa ajili ya kusafirisha kwenda kuilaza katika Hospitali Kuu ya Jeshi ya Lugalo, jijini.
Jumla ya magari saba yalitumika kubebea miili hiyo, kila moja ikibeba miili miwili na kusindikizwa na kundi la wanajeshi.
Akizungumza kabla ya kuanza safari hiyo ya kwenda Hospitali ya Lugalo, Dk. Mwinyi alisema miili hiyo inatarajiwa kuagwa Alhamisi katika viwanja vya Wizara ya Ulinzi, eneo la Upanga.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...