Na Daniel J. Mwambene, Afisa Habari Ileje
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Misitu (TFS) imeamua
kuanzisha Shamba la Miti la Iyondo - Mswima ukiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi
ya 2015/2020 ibara ya 31 vifungu vya b,c,d,e na f kuhusiana sekta ya Maliasili.
Kwa mujibu wa Meneja wa Mradi wa Iyondo-Mswima Ndg. Deograsian Kavishe
upandaji miti utaanza rasmi katika mwaka wa Fedha 2018/2019 ikiwa baadhi ya
kazi zilianza kutekelezwa na Mradi katika mwaka wa fedha 2017/2018.
Kuanzishwa kwa shamba hili la Katengele kunaifanya Tanzania kuwa na
mashamba ya miti ya kupandwa 23 yakiwa yanapatikana katika Kanda
mbalimbali kati ya hayo manne yapo katika hatua ya uanzishwaji likiwemo
hilo la Iyondo-Mswima wilayani Ileje.
Kutokana na soko hili kuwa ndani ya msitu wa hifadhi na ili kufikia
malengo yaliyokusudiwa kwa kufuata Kanuni, Sheria na taratibu za
uanzishwaji na uendeshaji wa miradi ya upandaji miti hapa nchini, soko
hilo halistahili kuendelea kuwepo mahali lilipo, hivyo linatakiwa
kuhamishiwa sehemu nyingine nje ya hifadhi zikiwemo kaya 13
zinazoishi ndani ya eneo hilo. Ujenzi wa miundombinu katika eneo
lililochaguliwa utafanywa na serikali kupitia wakala wa Misitu (TFS).
Ili kuendeleza mahusiano mazuri na wadau mbalimbali wa maendeleo TFS imeshirikisha
Baraza la Madiwani, wataalam wa Halmashauri pamoja na Serikali Kuu.
Michakato hiyo ilianzia kwenye vikao vya CMT, Kamati ya Uchumi Ujenzi na
Mazingira, Kamati ya Fedha Uongozi na Mipango pamoja na Baraza la
Madiwani ambalo liliridhia kuhama kwa Mnada wa Soko hilo kutoka mahali
lilipo na kwenda sehemu nyingine.
Baraza la Madiwani baada ya kujadili na kupitia mapendekezo ya vikao vilivyotangulia
kisheria liliridhia juu ya kuhama kwa soko la Katengele kutoka mahali lilipo na kwenda
Njiapanda ya Shule ya Msingi Mbangala katika barabara ya Ibaba - Katengele ili
kupisha uanzishwaji wa Mradi wa Shamba la Miti la Iyondo - Mswima.
Makubaliano hayo yalifikiwa baada ya upigaji kura kufanyika ambapo Wah.
Madiwani wane waliliridhia mnada wa Katengele uhamishiwe eneo la Ghala - Sange
huku Madiwani 18 wakiridhia Mnada wa Katengele uhamishiwe Njiapanda ya Shule
ya Msingi Mbangala.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ileje Ndugu Haji Mnasi (aliyesimama) akizungumza kwenye Baraza Maalum kuhusu Mnada wa Katengele
Eneo la Njiapanda ya Shule ya Msingi Mbangala panapotarajiwa kuhamishiwa Mnada wa Katengele.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ileje Mhe.Ubatizo Songa akiongoza Wahe. Madiwani na Wataalam wa Halmashauri ya Wilaya ya Ileje walipotembelea eneo la Mradiwa Upandaji Miti la Iyondo-Mswima.Chini ni kitalu cha miti kilichopo Katengele-Ileje kikitarajiwa kubadilisha sura ya msitu wa Iyondo-Mswima wilayani Ileje.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...