Na Rhoda James- Dar es Salaam.
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani ameagiza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ifikapo Novemba, 2018 wawe tayari wamesitisha uagizaji wa viunganishi vya miundombinu ya umeme (Accessories) kutoka nje ya nchi badala yake wanunue hapa hapa nchini.
Waziri Daktari Kalemani, ametoa agizo hilo leo tarehe 6 Agosti, 2018 wakati alipotembelea Kiwanda cha uzalishaji viunganishi cha Auto Mech Ltd kilichopo Tabata jijini Dar es Salaam ili kujionea uwezo wa Kiwanda hicho katika uzalishaji viunganishi hivyo.
“Nimekuja hapa ili kujiridhisha kama Kiwanda hiki kina uwezo wa kuzalisha viunganishi vya kutosha, nimejiridhisha kuwa, kiwanda hiki kina uwezo wa kuzalisha viunganishi hivyo, kwa hiyo nimetoa miezi mitatu ili TANESCO, REA na Wakandarasi wote kwa pamoja wajiandae sasa kunua vifaa hivi nchini.” Alisema Waziri Kalemani.
Akizungumza katika ziara hiyo alieleza kuwa, miezi mitatu iliyopita alisitisha uagizaji wa Mita za luku na Nguzo kutoka nje lakini baado kuna changamoto ya wananchi kuchelewa kuunganishiwa umeme na tatizo kubwa ni ukosefu wa viunganishi hivyo.
Pia Waziri Kalemani amesema kuwa, “nimeelezwa kuwa, kiwanda hiki kinauwezo wakuzalisha tani tano kwa siku ambapo ni kwa shifti moja lakini wana uwezo wa kuzalisha tani 15 kwa siku kwa shifti tatu”.
Aidha, Waziri Kalemani ameogeza kuwa manufaa ya kutembelea kiwanda hiki ni kujiridhisha kuwa kina uwezo mkubwa wa kuzalisha viunganishi hivyo na hatimae kuokoa gharama kubwa ya uagizaji viunganishi hivyo kutoka nje ya nchi.
“TANESCO, REA na Wakandarasi wamekuwa wakichukua miezi 6 kuagiza, miezi 3 kukamilisha taratibu za bandarini lakini sasa tukivinunua hapa nchini tutaokoa gharama kubwa na wananchi watapata ajira pamoja na kuunganishiwa umeme kwa wakati.” Alisema Waziri Kalemani.
Kwa nyakati tofauti Waziri Kalemani ametoa wito kwa Watanzania wenye uwezo wa fedha na wenye nia kuazisha viwanda vya namna hii ili kuonesha uwezo wa ndani.
Hali kadhalika, Kiwanda hiki kimeanzisha utengenezaji wa majiko ambayo yanatumia mabaki ya mbao badala ya kutumia mkaa ambao sio rafiki na mazingira, lakini sasa tunaokoa mazingira kwa kutumia nishati hii mbadala.
Kwa upande wake, Meneja wa Kiwanda hicho Mhandisi Frimos Mselle amesema kuwa, Kiwanda hiki kina uwezo mkubwa wa kuzalisha viunganishi hivi na wanaahidi na kuhakikisha Serikali kuwa, viunganishi hivyo vinapatikana kwa urahisi na vya kutosha.
 Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (kushoto mstari wa mbele) akieleza jambo wakati akikagua Viunganishi vya miundombinu ya Umeme vinavyotengenezwa katika Kiwanda cha Auto Mech Limited kilicho Tabata jijini Dar es Salaam.  Wengine katika picha ni Viongozi Waandamizi kutoka Wizara ya Nishati, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Wakala wa Nishati Vijijini, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) na Viongozi kutoka kiwanda cha Auto Mech limited.
 Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (kushoto) akikagua vyuma ambavyo vinatengenezwa kwenye kiwanda cha Auto Mech Limited kilichopo Tabata jijini Dar es Salaam.
 Baadhi ya Mashine na Vifaa ambavyo vinatengenezwa kwenye kiwanda cha Auto Mech Limited kilichopo Tabata jijini Dar es Salaam.
Meneja wa kiwanda cha Auto Mech Limited, Mhandisi Frimos Mselle (mwenye koti la jano) akitoa maelezo kwa Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (wa pili kulia) wakati alipotembelea kiwanda hicho.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...