JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
OFISI YA MAKAMU WA RAIS
 
 
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Ndugu January Makamba (Mb), leo anaanza ziara ya mikoa 19 nchini, ambayo itafanyika kwa awamu tatu. Ziara hiyo inamadhumuni yafuatayo:- 

1. Kukagua, kutathmini na kuzungumza na viongozi, wataalam, watendaji na wananchi wa mikoa husika kuhusu maeneo yanayopendekezwa kuhifadhiwa kwa mujibu wa Sheria ya Mazingira. 

Kama inavyofahamika, Sheria ya Mazingira, hasa vifungu vya 47, 51, 54, 56, na 58 (3), inatoa mamlaka kwa Waziri mwenye dhamana ya mazingira kutangaza, kutamka au kuamuru, kupita kwenye Gazeti la Serikali, baadhi ya maeneo nchini kuwa ni Maeneo Lindwa Kimazingira (Environmental Protected Area) au Maeneo Nyeti Kimazingira (Environmental Sensitive Area). 


Nyenzo hizi zimewekwa ili kuyalinda maeneo muhimu kwa mifumo ya kiikolojia (ikiwemo vyanzo vya maji, mito, maziwa, mabwawa, milima na vilima, chemichemi, ardhi oevu, mazalia ya samaki, misitu, nk.) ambayo hayana ulinzi wa Sheria nyingine. Sheria imeweka vigezo kwa maeneo hayo.

 Ofisi ya Makamu wa Rais, kupitia Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), iliomba na kupokea kutoka katika Halmashauri mbalimbali nchini mapendekezo ya maeneo hayo. Jumla ya maeneo 77 yalipendekezwa, ikiwemo vyanzo muhimu vya maji, mazalia ya samaki na wanyama adimu, maeneo ya ardhi oevu, mabwawa, mito na chemichemi nyeti. Mikoa iliorodhesha maeneo hayo kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa na Sheria. Katika awamu ya kwanza, maeneo takriban 20 yanatarajiwa kuhifadhiwa kwa kutumia Sheria ya Mazingira. 

Katika ziara yake, Ndugu Makamba anatarajia kuyaona maeneo hayo, kutathmini hoja na haja ya kuyahifadhi na kuzungumza na viongozi wa mikoa, halmashauri na wananchi katika maeneo hayo ilikubaini utayari na uwezo wao katika kusimamia uhifadhi mara maeneo hayo yatakapotangazwa. Vilevile, katika ziara hiyo, Ndugu Makamba atapokea mapendekezo ya maeneo mapya hasa pale ambapo mapendekezo yaliyotolewa awali hayakutokana na ushirikishwaji mpana. Orodha ya maeneo yanayopendekezwa itatolewa kadri ziara inavyoendelea katika kila mkoa. 


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...