Benki kuu ya Tanzania (BoT) inakanusha taarifa potofu zinazozosambazwa kupitia mitandao mbalimbali ya kijamii zikidai kuwa Benki Kuu imechapisha noti zenye thamani ya shilingi trilioni 1.5 kwa ajili ya matumizi ya serikali.


Benki Kuu inauarifu Umma kuwa, taarifa hiyo sio sahihi na inalenga kuathiri imani ya Wananchi na wadau wa kimataifa kuhusu uthabiti wa fedha ya Tanzania. Aidha, Benki Kuu inawaasa Wananchi kuwa utoaji wa taarifa potofu kuhusu sekta ya fedha unaweza kuleta athari kubwa kwa mwenendo wa uchumi. Hivyo ni vyema Wananchi wajue yafuatayo kuhusu utoaji wa fedha kwa matumizi ya Serikali:


  • Mapato ya serikali hayawiani moja kwa moja na matumizi yake mwezi-hadi-mwezi. Kuna wakati mapato yanakuwa makubwa mfano miezi ya mwisho wa robo mwaka na wakati mwingine yanakuwa madogo. Kwa sababu ya kupishana kwa mapato na matumizi ya serikali, sheria imeruhusu serikali kuchukua mkopo wa muda mfupi kutoka Benki Kuu ili kuziba pengo pale linapotokea na kurejesha baadaye. Utaratibu huu unatumika duniani pote na hapa Tanzania sheria inairuhusu Serikali kukopa kutoka Benki Kuu kwa vipindi vifupi hadi ukomo wa asilimia 12.5 ya mapato ya ndani ya serikali ya mwaka uliotangulia.


  • Ili kupata picha halisi ya utekelezaji wa bajeti ya serikali na hali ya deni la Taifa, ni vyema kuangalia mwenendo mzima katika kipindi cha miezi kumi na mbili ya mwaka wa fedha husika, badala ya kuangalia mwezi mmoja mmoja, ambapo kuna mabadiliko ya kimsimu. Mtazamo wa mwaka mzima hutoa uhalisia wa mapato na matumizi, na ongezeko la deni lililohitajika kuwezesha utekelezaji wa bajeti ya serikali katika kipindi hicho. Taarifa ya kila mwezi ya uchumi ya Benki Kuu toleo la mwezi Julai inaonesha kwamba mkopo wa muda mfupi (overdraft) wa Benki Kuu kwa serikali uliongezeka kutoka shilingi bilioni 610.0 mwezi Mei 2018 hadi shilingi bilioni 1,937.4 mwezi Juni 2018, sawa na ongezeko la shilingi bilioni 1,327.4. Ongezeko hili halipaswi kuangaliwa kama tukio la mwezi Juni 2018 pekee kwani taarifa hiyohiyo inaonesha kuwa kati ya mwezi Juni 2017 na mwezi Mei 2018 overdraft ya Benki Kuu ya Tanzania kwa serikali ilipungua kwa shilingi bilioni 936.6, kutoka shilingi bilioni 1,546.6 hadi shilingi bilioni 610.0.  Kupungua huku kulichangiwa na mapato ya kawaida ya serikali pamoja na mikopo kutoka nje ya nchi.


  • Aidha, Benki Kuu haijachapisha noti mpya katika kipindi hiki, hata hivyo noti mpya, hazichapishwi kiholela ili kutoa pesa kwa serikali, bali huchapishwa kulingana na taratibu za kisheria. Kwa kawaida utengenezaji wa noti na sarafu huanza baada ya kukamilika kwa mchakato wa usanifu wa michoro, aina ya karatasi itakayotumika, alama za utambulisho wa nchi pamoja na alama za usalama. Na mara baada ya kukamilika kwa mchakato huo, Benki Kuu huandaa kiasi gani kitakachoweza kutosheleza mahitaji ya nchi kwa kipindi maalum kwa kuzingatia ukuaji wa pato la Taifa, Mfumuko wa bei na pia kufidia fedha zilizochakaa ambazo hazipaswi kurudi katika mzunguko na kiasi kilichobaki (buffer stock) ili kutosheleza kipindi chote cha mchakato wa uchapishaji.
Benki kuu inawaasa Wananchi kutotoa taarifa zisizo za kweli zenye lengo la kuupotosha Umma na kusababisha hofu na kupoteza imani juu ya uthabiti wa fedha ya Tanzania na badala yake wawe wanaomba kupewa taarifa kutoka Taasisi husika.


BENKI KUU YA TANZANIA


Idara ya Uhusiano wa Umma na Itifaki

11 Septemba, 2018

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...