Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani 
Frank Mvungi- MAELEZO, Dodoma
SERIKALI  imetumia kiasi cha shilingi bilioni 216 kukamilisha mradi wa Umeme wa Makambako hadi Songea ikiwa ni moja ya miradi ya kimkakati yenye lengo ya kufanikisha sera ya Tanzania ya viwanda.

Akizungumza katika kipindi cha TUNATEKELEZA, Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani amesema kuwa ifikapo mwisho wa mwezi Septemba mitambo ya mradi huo itawashwa na wananchi wa mikoa ya Njombe na Ruvuma wataanza kufurahia umeme wa uhakika kutoka gridi ya taifa. 

"Mradi huu utakuwa na manufaa makubwa kwa wananchi kwani wataunganishiwa umeme kwa bei nafuu ya mradi wa REA ambayo ni elfu 27 tu na kuwanufaisha wateja 22,700 hali itakayowawezesha wananchi kutumia umeme huo kwa ujenzi wa viwanda na shughuli za maendeleo katika maeneo yao" Alisisitiza Dkt. Kalemani

Akifafanua zaidi Dkt. Kalemani amesema kuwa kukamilika kwa mradi huo kutaokoa fedha kiasi cha Shilingi bilioni 9.1 ambazo zinatumika kununua mafuta mazito yanayotumika kwenye mitambo ya kuzalisha umeme iliyopo Madaba, Ludewa, Mbinga, Namtumbo na Songea Mjini. 

Akielezea ujenzi wa mradi huo uliotekelezwa na Serikali ya Tanznaia kwa kuhsirikiana na Serikali ya Sweden, Waziri Kalemani amesema mradi huo umetekelezwa kwa awamu mbili. "Sehemu ya kwanza ya mradi huu imehusisha ujenzi wa vituo vitatu vya kupooza na kusambaza umeme mkubwa wa msongo wa KV 220 vilivyojengwa Makambako, Madaba na Songea na sehemu ya pili ilihusisha ujenzi wa miundo mbinu ya kusafirisha umeme". 

Akizungumzia mradi wa REA awamu ya tatu ambao unatarajiwa kuunganisha vijiji 5100 kwenye mtandao wa umeme Dkt. Kalemani amesema vijiji 818 tayari vimeshaunganishwa tokea kuanza kwa mradi huo mwezi Julai mwaka huu. 

Aliongeza kuwa lengo la Serikali kufikisha umeme katika Vijiji 12,268 ni kutekeleza azma ya kufikisha umeme kwa kila mwananchi bila kujali anaishi mjini au kijijini ikiwa ni utekelezaji wa ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM).

Kwa upande wa mradi wa Kinyerezi Dkt. Kalemani amesema mradi huo umekamilika kwa asilimia 100 na megawati 218 tayari zimeshaingizwa kwenye gridi ya Taifa. Megawati za umeme zilizobaki zinatarajiwa kuingizwa kwenye gridi ya taifa kabla ya mwanzo wa mwezi Oktoba.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...