Na Joseph Msami

Isaac Gamba, ni kweli umetutoka? Majina yako yenye kishindo yakitamkwa yamekataa kutoka moyoni mwangu. Isaac Nyagabona Malibwa Muyenjwa Gamba! Najuta kwanini sikuongea nawe uliponiita kama tunavyoitana Muye, siku ya Oktoba 10, nilikujibu haraka Muye Baba, kisha nikawaza kuwa tutaongea siku za hivi karibuni. Sikukupigai wala hukunipigia hadi napata taarifa eti umefariki.

Nakumbuka sana maongezi yetu ya zaidi ya saa moja hadi pale chaji ya simu iliponiishia, kibwagizo chako cha Muye Baba, pale unapobaini kuna jambo limetokea, hakiachi kuusumbua moyo wangu.

Mara ya mwisho tulionana ulivyokuja likizo miezi michache iliyopita, na tukazumgumza mengi ikiwamo mipango ya kukuza taaluma yetu kimataifa. Naikumbuka sana kauli yako, kwamba unapanga baada ya miaka mitano ya kutumika na kituo cha DW Ujerumani, utarejea nyumbani.

Miongoni mwa mambo uliyoniachia ni moyo wa kujiamini, ujasiri na uthubutu. Ulipotaka kumiliki gari, ulinishirikisha na tuliomba nyumbani kwako pale Sinza karibu na kituo cha ITV na kisha ukanishirikisha kwamba unaanza kukusanya shilingi kuanzia 10,000. Kisha ulivyomiliki uliniita tena kwa maombi.

Hata safari ya Ujerumani tuliianza kwa msingi wa maombi.Mlipoelekea nyumbani kwa likizo kutoka Mrekani, uliniita ukaniendesha hadi Mlimani City, tulifanya maombi na ukanieleza adhma yako ya kutaka kufanya kazi kimataifa.

Hulka ya shukrani, uliyokuwa nayo imenifunza mengi rafiki Gamba, kwani siku ulipopata DW, ulinipigia na kunieleza ulivyofurahi na tukamshukuru Mungu pamoja na ulisisitiza tushukuru palepale tulipoomba yani kwenye gari na tulifanya hivyo.

Maneno hayawezi kutosha kueleza, lakini siwezi kuacha kukumbuka ulivyonialika Bonne, tena ulinitania kwamba kutoka New York unakula mwewe kirahisi sana hapo, ‘au unataka kuja na ndinga’’? Ukimaanisha gari na kama kawaida ulimalizia kwa kicheko.

Tangulia Gamba, Bwana alitoa, Bwana ametwaa, jina la Bwana libarikiwe!

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...