Na Teresia Mhagama, Dodoma
IMEELEZWA kuwa, matumizi ya gesi asilia katika kuzalisha umeme yameokoa fedha za kigeni kiasi cha Dola za Marekani bilioni 10.29 ambazo zingetumika kununua mafuta nje ya nchi kwa ajili ya kuzalisha umeme kutoka mwaka 2004 hadi Septemba 2018.

Hayo yameelezwa jijini Dodoma na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Eng. Kapuulya Musomba wakati akiwasilisha taarifa kuhusu mchango wa Gesi asilia katika uzalishaji wa umeme kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini.

“ Kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2004 hadi Septemba 2018, Gesi asilia kiasi cha futi za ujazo bilioni 381 kilitumika kuzalisha umeme pekee ambapo hadi kufikia mwezi Septemba 2018, mitambo yenye uwezo wa kuzalisha umeme wa jumla ya megawati 831 kwa siku kutokana na gesi asilia imewekezwa nchini,” alisema Musomba.

Aliongeza kuwa, zaidi ya asilimia 50 ya umeme unaozalishwa nchini, unatokana na Gesi asilia huku vyanzo vingine vya uzalishaji umeme vikiwa ni maji, nishati jadidifu na mafuta.

Kwa upande wake, Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani, akitoa taarifa ya utangulizi kwa Kamati hiyo, alisema kuwa kiasi cha gesi kilichopatikana nchini hadi sasa ni futi za ujazo trilioni 57.54 ambapo futi za ujazo trilioni 8.96 zimepangwa kutumika kuzalisha umeme hadi ifikapo mwaka 2046.

Alisema kuwa, Serikali inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia ukiwemo mradi wa upanuzi wa kituo cha kuzalisha umeme cha Kinyerezi I kwa kuongeza mitambo itakayozalisha megawati 185 na kufanya kituo hicho ambacho kwa sasa kinazalisha megawati 150, kuweza kuzalisha jumla ya megawati 335.

“ Tunatarajia pia kutekeleza mradi wa Somanga Fungu utakaozalisha umeme wa kiasi cha megawati 330 kwa kutumia Gesi asilia unaotarajiwa kukamilika mwaka 2021 ambapo mahitaji ya Gesi asilia katika mtambo huu yatakuwa takriban futi za ujazo milioni 46 kwa siku,” alisema Dkt. Kalemani.

Vilevile alisema kuwa, Gesi asilia itatumika kuzalisha umeme wa kiasi cha megawati 300 mkoani Mtwara ambapo mradi huo utakamilika mwaka 2021 na matumizi ya gesi asilia katika mtambo huo yatakuwa ni takriban futi za ujazo milioni 42 kwa siku.
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (aliyesimama) akitoa taarifa ya utangulizi kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu mchango wa Gesi asilia katika uzalishaji wa umeme jijini Dodoma.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Eng. Kapuulya Musomba akiwasilisha taarifa kuhusu mchango wa Gesi asilia katika uzalishaji wa umeme kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini jijini Dodoma.
Baadhi ya watumishi wa Wizara ya Nishati, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) wakifuatilia kikao baina yao na Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini jijini Dodoma.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...