Na Leandra Gabriel, Blogu ya jamii

SERIKALI  imesema kuwa katika kukabiliana na uhifadhi mazingira ni wakati muafaka kwa wadau  kuwekeza katika uzalishaji wa mifuko mbadala  ambayo haina madhara  katika  utunzaji wa mazingira.
Akizungumza katika kikao kilichohusisha wadau wa mazingira kuhusu fursa za uwekezaji  katika uzalishaji wa mifuko mbadala, Naibu katibu  mkuu  Ofisi ya Makamu wa Rais, Balozi Joseph Edward Sokoine  amesema kuwa malengo ya kikao hicho ni kujadili mabadiliko katika uhifadhi ya mazingira  pamoja na kujadiliana na wadau juu ya namna bora ya kutokomeza matumizi ya mifuko ya plastiki kwa kutengeneza mifuko mbadala ya karatasi au nguo
Balozi Sokoine amesema kuwa hiyo ni fursa kwa wajasiriamali kuwekeza katika uzalishaji wa mifuko ya karatasi na nguo ili kuchangia katika uhifadhi wa mazingira na kuongeza kipato chao na kipato ha taifa kwa ujumla.
Balozi Sokoine  amesema kauli mbiu ya "Mifuko mbadala kwa ustawi wa afya, mazingira na uchumi wetu" itumike katika kuhamasisha namna bora ya utunzaji wa mazingira kwa jamii kwa ujumla.
Balozi Sokoine  amesema kuwa mifuko mbadala iwe na gharama nafuu na amewataka wadau wa mazingira kuendeleza kampeni ya kutokomeza matumizi ya mifuko na plastiki ambayo inachangia katika  uchafuzi wa mazingira.
Kwa upande wake Mhandisi kutoka Wizara ya Viwanda, Idara ya Mazingira, Ofisi ya Makamu wa Rais Julius Enock amesema kuwa athari  za mifuko ya plastiki ni kubwa sana na hudumu kwa muda mrefu zaidi.
Amesema kuwa takribani mifuko bilioni 7.8 hadi 10 hutumika  kwa mwaka nchini na mifuko hiyo hudumu ardhini kwa miaka 500 hadi 1000 huku ikiendelea kuathiri mazingira.
 Amesema kuwa mifuko iliyozalishwa 1950 kwa mara ya kwanza bado ipo ardhini  ikiendelea kuathiri mazingira kwa kiasi kikubwa huku akitaja athari nyingine ikiwa ni pamoja na  kuathiri shughuli za kitalii, kuuwa mifugo na viumbe vya baharini hali ambayo hupelekea kuathiri kipato cha mtu mmoja mmoja na Serikali kwa ujumla.
Julius amesema kuwa asilimia 60 hadi 80 ya taka za plastiki huishia baharini na mkakati wa kutokomeza janga hili ni  kwakila mtu kutimiza wajibu wake katika ulinzi wa mazingira .

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...