Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii
MAMLAKA ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA) imeendelea kuwapokea na kuwarudisha huduma ya maji kwa wateja waliokatiwa huduma hiyo kutokana na kushindwa kulipa bili zao.
Hatua hiyo imekuja baada ya DAWASA kuanzisha kampeni mpya ya 'Dawasa Tunawahitaji' inayowataka wateja wote wa zamani kurudishiwa huduma za maji na wakubaliane watalipa katika mfumo gani.
Kampeni hiyo iliyozinduliwa na Ofisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Mhandisi Cyprian Luhemeja amesema kuwa kampeni ya ' Dawasa Tunawahitaji' lengo kuu ni kuona wateja wote takribani 10000 waliokatiwa maji wanaanza kupata tena huduma hiyo.
Luhemeja alisema kuwa amewaagiza maafisa wote wa utawala wafanye hivyo haraka,lengo la 'Dawasa Tunawahitaji' ni kuwatafuta wateja wa zamani na wapya ili waunganishiwe maji na hiyo ni kampenibya kudumu.
Kampeni hiyo itawahusisha wateja wote waliokatiwa huduma ya maji na kupitia kwa mameneja wa mikoa yote ya DAWASA kwa pamoja wakubaliane watalipa kwa miezi mingapi madeni ambayo wanadaiwa.
Kwa upande wa mameneja kutoka Mikoa mbalimbali ya DAWASA , wamethibitisha wateja wenye madeni ya muda mrefu kuanza kwenda kwenye ofisi zao kukaa nao chini na wakubaliane katika ulipaji.
Meneja Mkoa wa Kinondoni amethibitisha hilo na kusema muitikio wa watu umeanza kuwa mkubwa na wengi wakionekana kuelewa lengo la Mamlaka katika kuhakikisha watu wote wanatumia maji safi na salama kupitia kampeni ya Tunawahitaji.
Na kutoka ofisi za Boko, wateja 16 tayari wamesharudishiwa huduma ya maji baada ya kukaa pamoja baina ya DAWASA na wateja na wamekubaliana namna ya kulipa madeni yao huku wengine wakiendelea kujitokeza.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...