Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng; Atashasta Nditiye akiongea na waandishi wa habari kuhusu dhima ya ziara aliyoifanya kwa ofisi za Makao Makuu ya Halotel jijini Dar es Salaam kulia ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Halotel Nguyen Van Son. 
Makamu wa Kitengo cha Idara ya Umeme wa kampuni ya Halotel, akitoa maelezo jinsi mfumo wa Umeme unavyofanya kazi kwenye kituo cha data kwa Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng; Atashasta Nditiye (Kushoto) na Mkurugenzi wa Kampuni ya Halotel Nguyen Van Son wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu waziri huyo katika ofisi za makao makuu za Halotel jijini Dar es Salaam. 
Pichani kati ni  Naibu Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi, Mhandisi Atashasta Nditiye  akimsikiliza  Mkurugenzi wa Kampuni ya Halotel Nguyen Van Son alipokuwa akifafanua jambo wakati wa kikao chao cha pamoja mara baada ya kufanya ziara ya kuitembelea kampuni hiyo ili kujua shughuli wanazozifanya katika kuwahudumia wateja pamoja na changamoto wanazokumbana nazo kila siku.
Kikao cha pamoja kikiendelea


 
· Yaipongeza kutimiza ahadi ilizozitoa kwa serikali.

Kwa kutambua umuhimu na ukuaji wa sekta ya mawasiliano nchini Tanzania, serikali imeiahidi kampuni ya mawasiliano ya Halotel kuendelea kushirikiana nayo katika kutatua changamoto wanazozikabili kwa pamoja.

Hayo yalisemwa wakati wa ziara maalum ya Naibu Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi, Mhandisi Atashasta Nditiye wakati alipoitembelea kampuni hiyo ili kujua shughuli wanazozifanya katika kuwahudumia wateja pamoja na changamoto wanazokumbana nazo kila siku.

“Lengo la ziara hii ni kuja kuwasikiliza, kujua shughuli mnazozifanya pamoja na changamoto mnazokumbana nazo. Serikali inatambua ukuaji na umuhimu wa sekta ya mawasiliano katika kuchangia uchumi. Na wadau wakubwa katika sekta hii ni makampuni ya simu kama Halotel. Hivyo hatuna budi kuyatembelea, kuongea nayo, kuyasikiliza na kushirikiana nao wapi tufanye kipi kama serikali katika sekta nzima ya mawasiliano. Ningependa kuwatoa hofu kwamba kama serikali tuko pamoja nao,” alisema Mhandisi Nditiye.

“Serikali inatambua sana mchango wa makampuni ya simu na ndiyo maana tumeamua kuwatembelea ili kujua shughuli wanazozifanya. Kwa mfano, mbali na kuzungumza na kusikiliza changamoto zao lakini nimepata fursa ya kutembelea kitengo chao wanacho hudumia wateja, mitambo na kitengo chao wanakitumia kufanyia huduma za kifedha. Nimezisikiliza changamoto zao na ninaahidi kwenda kuzifanyia kazi,” alihitimisha Mhandisi Nditiye.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halotel Nguyen Van Son, aliezea mafanikio ambayo kampuni yake imeyafikia mojawapo ikiwa ni ahadi ilizozitoa kwa serikali katika utoaji wa huduma nchini.

“Katika utoaji wa huduma za mawasiliano Tanzania tulitoa ahadi kadhaa kwa serikali na ningependa kuchukua fursa hii kuifahamisha serikali kuwa tumetekeleza kwa kiasi kikubwa. Tuliahidi kutoa huduma za mtandao wa intaneti katika shule 450 na tumevuka lengo kwa 455. Tuliahidi kutandaza kebo za huduma ya intaneti katika ofisi za mabaraza ya wilaya 150 na tumefanikiwa kwa kufikia ofisi 147. Pia kusambaza miundombinu ya mawasiliano ya fibre katika hospitali za wilaya 150 na tumefanikiwa zote 150. Tuliahidi kusambaza miundombuni ya mawasiliano ya fibre kwa vituo vya polisi vya wilaya 150 na tumefanikiwa 121. Lakini pia, tuliahidi kusambaza miundombinu ya mawasiliano ya fibre katika vituo vya ofisi za posta za wilaya 65 na tumevuka kwa kufunga 66,” alisema na kuongezea Son.

Licha ya mafanikio hayo ambayo Halotel imeyafanikisha kwa kutimiza ahadi ambazo iliipatia serikali, kampuni hiyo ilielezea changamoto kadhaa inazokumbana nazo.

“Ili kutimiza dhima yetu ya kuhakikisha kila Mtanzania anafikiwa na huduma za mawasiliano kwa bei nafuu lakini pia tunakumbwa na changamoto kadhaa. Mojawapo ni pamoja na kuharibiwa kwa mifumo yetu ya miundombinu ya mawasiliano na baadhi ya wananchi ambao sio waaminifu katika baadhi ya mikoa. Vitendo hivi si tu vinakwamisha juhudi zetu za kufikisha mawasiliano katika kila pembe ya nchi lakini pia inawazuia wananchi kufikiwa na huduma zetu hivyo kukwamisha shughuli za mawasiliano na uchumi. Tungeomba katika hili serikali kushirikiana nasi ili kuzuia vitendo hivi vya kihalifu na kujenga hamasa juu ya umuhimu wa mitambo hii,” aliongezea Son.

“Pia tunaiomba serikali kushirikiana na Halotel katika kupambana na changamoto ya wizi wa mitandaoni. Kama mnavyojua huduma za mawasiliano hususani huduma za fedha kwa njia ya simu za mkononi yanatumika kwa kiasi kikubwa katika kurahisisha shughuli mbalimbali. Wahalifu wa mitandaoni nao wanaoitumia fursa hii kuwalaghai wateja hivyo kuvunja uaminifu baina yetu. Halotel inapendekeza kuwepo na ushirikiano na serikali katika kulikabili hili na kulitatua kwa pamoja. Tunapendekeza kuwepo kwa vikao, semina au warsha za mara kwa mara ili kupanga mikakati na kumaliza kabisa changamoto hii,” alihitimisha Son.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...