Na Issa Mtuwa, Dodoma 
Uongozi wa Kampuni ya Acacia kupitia Mgodi wa North Mara umezungumza na Serikali kuelezea hatua zilizochukuliwa hadi sasa kudhibiti maji yenye sumu ikiwa ni wiki moja tu ipite tangu Waziri wa Madini Doto Biteko, atangaze kufunga shuguli za mgodi huo endapo utashindwa kudhibiti maji ya sumu yanayotiririka kwenye makazi ya watu, ifike Machi 30 mwaka huu.
Tamko hilo la serikali limeifanya kampuni ya Acacia kuchukua hatua za haraka za kudhibiti maji hayo ili kukwepa rungu la serikali la kuufunga mgodi huo.  Machi 12, uongozi wa Acacia North Mara ulikutana na Waziri Biteko ofisini kwake jijini Dodoma kwa lengo la kueleza hatua iliyofikiwa ya kutekeleza agizo la serikali. 

Uongozi wa kampuni hiyo ukizungumza katika kikao hicho, ulieleza kuwa, tayari mgodi huo umechukua hatua za haraka tangu kutolewa kwa agizo na kwamba hadi sasa suala la kudhibiti maji yenye sumu limeshetekelezwa na hakuna maji yanayotiririka kuelekea kwenye makazi ya watu.
Aidha, ulimweleza kuwa, pamoja na kudhibiti maji hayo kupitia bwawa la kuhifadhia maji yenye sumu yajulikanayo kitaalam kama “topesumu” (Tailings Storage Facility- TSF) mgodi umeanza kuchukuwa hatua za kujenga TSF mpya. 

“Mhe. Waziri tumekuja kutoa mrejesho wa utekelezaji wa agizo lako, tunafurahi kukuambia kuwa tumetekeleza agizo hilo na kwa sasa hakuna maji yanayotiririka. Pamoja na hatua hiyo mgodi umeanza mchakato wa ujenzi wa bwawa jipya (TSF) la kuhifadhia topesumu,” walieleza.

Aidha, ulimweleza Waziri Biteko kuhusu hujuma za uharibifu wa miundombinu ya bomba la maji yenye sumu unaofanywa kwa maksudi na wakazi wanaozunguka mgodi ili kufifisha juhudi zao za kudhibiti maji hayo wakiwa na lengo la kuufanya mgodi uonekane haujachukuwa hatua kudhibiti jambo hilo, ambapo walionesha picha mbalimbali ya namna bomba lilivyo pasuliwa ili maji yatiririke kuelekeka kwa wananchi.

Akizungumza katika kikao hicho, Waziri Biteko alieleza kuwa, amepokea taarifa ya kampuni husika na kuwapongeza kwa hatua zilizochukuliwa na kusema kuwa, ukweli wa jambo hilo atauthibitisha mara baada ya kupata ripoti ya wataalam watakaokwenda kuhakikisha kuhusu utekelezaji wa agizo hilo na kuongeza,“katika hili sitanii juu ya kuufunga mgodi ikiwa utashindwa kudhibiti tope sumu,”.

 “Naomba nirudie tena katika hili sitanii, sitabadilisha msimamo wangu kama serikali na utaendelea kubaki pale pale dawa pekee ni kutekelezwa kwa agizo hilo. Lakini niseme ukweli, nasikitishwa sana na kitendo hiki cha wananchi kupasua bomba, kwa hili sikubaliani nao na siwaungi mkono.
 Pia, aliongeza kuwa, atawasiliana na Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya kuona namna ya kudhibiti hali hiyo ili wale watakao bainika wachukuliwe hatua.

Waziri Biteko alilitoa agizo hilo   Machi 6, alipoutembelea mgodi huo hapo kwa ziara ya kikazi  pamoja na kuzungumza na wananchi kwenye mkutano wa hadhara katika kijiji cha Nyamongo wilaya ya Tarime.  
Waziri wa Madini Doto Biteko akiwa na viongozi wa Kampuni ya Acacia wa mgodi North Mara, ofisini kwake jijini Dodoma. Kulia ni Mbunge wa Viti Maalumu mkoa wa Mara, Agness Marwa. 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...