Na Teresia Mhagama,

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, chini ya uenyekiti wa Mariamu Ditopile Mzuzuri, imefanya ziara ya kikazi mkoani Iringa iliyokuwa na lengo na kukagua kazi ya utekelezaji wa mradi wa usambazaji umeme vijijini ili kijiridhisha endapo fedha zinazoidhinishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

Kamati hiyo ilikagua utekelezaji wa mradi wa usambazaji umeme vijijini wa Awamu ya Tatu (REA III) katika Kijiji cha Ngano, wilayani Iringa na katika Kitongoji cha Ikuvala kilichopo wilayani Kilolo ambapo waliambatana na Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu, Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Richard Kasesela, Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga na watendaji kutoka TANESCO.

Pamoja na kukagua utekelezaji wa mradi huo, Kamati hiyo ilipata fursa ya kuwasha rasmi umeme katika Kisima cha Maji, Shule ya Msingi na Zahanati katika Kijiji cha Ngano wilayani Iringa pamoja na kuwasha umeme katika Kitongoji cha Ikuvala, wilayani Kilolo.

“ Tunaipongea Wizara kwa kuzingatia agizo la Kamati ya Bunge la kuhakikisha kuwa umeme unafika katika Taasisi za Umma na Kijamii, kwani wakati tunakagua mradi huu mwaka jana, tuliongelea suala la wigo wa wakandarasi na tuliwashauri kwamba umeme ufike katika Taasisi za kijamii ikiwemo zahanati na Shule,” alisema Mzuzuri.

Mzuzuri alisema kuwa, haitaleta maana kama Wakandarasi wa umeme wa vijijini watasambaza umeme katika makazi ya watu pekee kisa tu wako katika wigo waliopangiwa na kuacha Taasisi muhimu za kijamii hivyo aliipongeza Wizara ya Nishati kwa kuitikia agizo hilo la Kamati na kulifanyia kazi.

Aidha, Kamati hiyo ya Bunge imeipongeza Wizara ya Nishati, kwa kufanyia kazi ushauri wa kupunguza bei za umeme ambapo sasa bei ya kuunganisha umeme vijijini ni 27,000 tu, iwe kwa miradi inayotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) au TANESCO.

“ Sisi kama Kamati tunapata faraja, pale tunapotoa ushauri na nyie mnaufanyia kazi, tunawatia moyo muendelee kufanya kazi kwa bidii ili mradi yale tunayoyapanga kwa pamoja yaweze kufanikiwa zaidi na zaidi,” alisema Mzuzuri.

Akitoa taarifa ya usambazaji umeme vijijini mkoani Iringa, Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu, alisema kuwa vijiji 179 mkoani humo vimepangwa kupelekewa umeme kupitia miradi mbalimbali ikiwemo wa REA III na mradi wa Backbone ambapo gharama zake ni takriban shilingi bilioni 30.

Naibu Waiziri alitumia fursa hiyo kuwakumbusha wananchi kuwa bei ya kuunganisha umeme vijijini ni shilingi 27,000 tu bila kujali kama mradi unatekelezwa na TANESCO au Wakala wa Nishati Vijijini kwani Serikali imedhamiria kurahisisha zoezi la kuwapelekea wananchi umeme.

Aidha, alilisisitiza kuhusu matumizi ya vifaa vya UMETA kwa wananchi vijijini na kuwataka wakandarasi kuhakikisha kuwa wanawapatia wananchi vifaa hivyo kwani baada ya kukamilika kwa mradi, Serikali itakagua endapo wakandarasi hao wametekeleza agizo hilo la Serikali.

Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini wakikata utepe kuashiria uzinduzi wa umeme katika Kitongoji wa Ikuvala wilayani Kilolo, Mkoa wa Iringa. Wa kwanza kulia ni Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu.
Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu, (katikati), akizungumza mbele ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini wakati walipofika katika Kijiji cha Ngano wilayani Iringa kukagua mradi wa usambazaji umeme vijijini wa Awamu ya Tatu. Wa Pili kushoto ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mariamu Ditopile Mzuzuri na Wa Tatu kulia ni Kaimu Kamisha wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mariamu Ditopile Mzuzuri akibonyeza kitufe kuashiria uzinduzi wa umeme katika Kitongoji wa Ikuvala wilayani Kilolo, Mkoa wa Iringa. Wa kwanza kulia ni Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...