Mheshimiwa Prof. Palamagamba J. Kabudi (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, leo tarehe 13 Machi, 2019 amekutana na kufanya mazungumzo na Mheshimiwa WANG Ke, Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China.

Mheshimiwa WANG Ke pamoja na masuala mengine amewasilisha kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki barua ya pongezi kutoka kwa Mheshimiwa Wang Yi, Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Watu wa China kufuatia Prof. Kabudi kuteuliwa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. 

Aidha Prof. Kabudi kupitia kwa Mheshimwa Balozi ameshukuru kwa salamu hizo za pongezi alizopokea.

Katika mazungumzo yao, Prof. Kabudi na Balozi WANG Ke, wameahidi kufanya kazi kwa pamoja ili kuimarisha ushirikiano wa kihistoria baina ya nchi hizo mbili. Na kwa pamoja wamesisitiza umuhimu wa kuendelea na jitihada za kuimarisha mahusiano ya kisiasa, kijamii, kiuchumi hususan kwenye maeneo la uwekezaji, biashara, utalii na miundombinu.
                                                                      
Prof. Kabudi ametumia fursa hiyo kuishukuru Jamhuri ya Watu wa China kwa misaada ya kimaendeleo wanayoendelea kuitoa na kwamba Serikali inafurahishwa na Jinsi China inavyounga mkono jitihada zake za kuwaletea wananchi maendeleo na kujenga uchumi.

Tanzania na China zimekuwa na mahusiano ya kidiplomasia tangu mwaka 1964 na mwaka huu zinatarajia kuadhimisha miaka 55 ya ushirikiano huo.

Mheshimiwa Wang amekuwa Balozi wa kwanza kuonana na Mhe. Kabudi tangu kuteuliwa kwake na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuiongoza Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma.
13 Machi 2019
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akipokea barua ya pongezi kutoka kwa Balozi wa China nchini, Mhe. WANG Ke. Balozi wa China aliwasilisha barua hiyo kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Mhe. WANG Yi ambapo anampongeza Prof. Kabudi kwa kuteuliwa kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Mhe. Prof. Kabudi akisoma barua ya pongezi kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa China ambayo iliwasilishwa wizarani na Balozi wa China nchini.

Mhe. Prof. Kabudi akiwa katika mazungumzo na Balozi wa China mara baada ya kupokea barua ya pongezi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...