*Aagiza taasisi zinazodaiwa malimbikizo kulipa mara moja 

Na Eline Maronga – HESLB, Kigoma

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Brigedia Jenerali (mstaafu) Emmanuel Maganga amewaagiza waajiri wote mkoani Kigoma ambao wanadaiwa malimbikizo ya makato ya mikopo ya elimu ya juu kuhakikisha wanawasilisha fedha hizo kwa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) mara moja.

Mkuu huyo wa mkoa ametoa maagizo hayo Jumanne, Machi 12, jioni wakati akikabidhi tuzo zilizotolewa na HESLB kwa waajiri watano bora mkoani Kigoma ambao wanatekeleza matakwa ya sheria ya HESLB kwa ufanisi.

“Nawapongezeni sana Bodi ya Mikopo, mnafanya kazi kubwa sana kwa taifa letu. Lakini nimeambiwa kuna baadhi ya taasisi hapa mkoani kwangu zinawakata wafanyakazi lakini hazileti kwenu fedha za makato, nimeshaelekeza wahakikishe fedha hizo zinalipwa mara moja,” alisema Brigedia Jenerali Maganga.

Kiongozi huyo, ambaye alikua mgeni rasmi katika hafla hiyo iliyofanyika katika Hoteli ya Lake Tanganyika, aliihimiza Bodi ya Mikopo kuhakikisha kila mnufaika wa mkopo ambaye hajajitokeza anasakwa na kuaSnza kurejesha.

“Akipatikana, wewe kata tu,” alisema na kuwapongeza wawakilishi wa waajiri kutoka taasisi tano ambazo ni Danish Refugee Council inayowasilisha Tshs 10.8 milioni kila mwezi kutoka kwa wanufaika 54.

Nyingine ni Norwegian Refugee Council inayowasilisha Tshs 7.3 milioni kwa mwezi kutoka kwa wanufaika 28; Diocese of Kigoma (CARITAS) yenye wanufaika tisa na inawasilisha Tshs 1.7 milioni kwa mwezi.

Nyingine ni Baba Watoto Centre for Youth and Children yenye wanufaika wanne na inayowasilisha Tshs 1.1 milioni kwa mwezi na taasisi ya Relief to Development Society (REDESO) yenye wanufaika 13 na inawasilisha Tshs 0.9 milioni kwa mwezi. 

Awali akimkaribisha Mkuu wa Mkoa katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Bw. Abdul-Razaq Badru alimweleza kiongozi huyo kuwa katika mwaka wa fedha 2017/2018, HESLB ilikusanya Tshs 181.4 bilioni na kuwa kutoka mkoa wa Kigoma pekee, zilikusanywa Tshs 2.66 bilioni (asilimia 1.4).

“Tunadhani tunaweza kukusanya zaidi kwa sababu tuna waajiri, wengine ni taasisi za Serikali, wanakata wanufaika lakini fedha hizo hazifiki kwetu … tumekuja kutoa tuzo lakini pia kuwahimiza waajiri sugu watimize matakwa ya sheria,” alisema Badru.

Akiwa mkoani Kigoma, Bw. Badru pia alipata fursa ya kuwasilisha mada kuhusu ‘Wajibu wa Waajiri katika Urejeshaji wa Mikopo’ kwa wajumbe wa Baraza la Ushauri la Mkoa wa Kigoma linalowajumuisha viongozi wote wakuu wa mkoa na wilaya.

Katika mada hiyo, Bw. Badru aliwakumbusha viongozi hao kuhusu wajibu wa waajiri kuhakikisha kuwa wanawasilisha kwa HESLB orodha ya waajiriwa wapya ndani ya siku 28 tangu wawaajiri kama sheria inavyoelekeza. 

“Wajibu mwingine ni kukata asilimia 15 ya mshahara ghafi wa mnufaika wa mkopo, na si chini ya hapo. Baada ya kukata, kila mwajiri anapaswa kuhakikisha anawasilisha makato hayo kwa Bodi ya Mikopo ndani ya siku 15 baada ya tarehe ya mwisho wa mwezi wa makato,” alifafanua Bw. Badru na kujibu maswali mbalimbali yaliyojitokeza.

HESLB ilianzishwa mwaka 2004 na kuanza kazi rasmi mwaka 2005 ikiwa na majukumu kadhaa, lakini makuu mawili – kutoa mikopo kwa wanafunzi wahitaji wa kitanzania waliopata nafasi za kujiunga na taasisi za elimu ya juu; na kukusanya mikopo iliyoiva iliyotolewa na Serikali tangu mwaka 1994/1995.
 Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Bregadia Jenerali Mstaafu Emmanuel Maganga akipokea tuzo ya Bodi ya kutambua mchango wake kwa waajiri wa Mkoa huo kutekeleza sheria ya Bodi.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu Abdul-Razaq Badiri akizungumza na waajiri waliotekeleza sheria ya Bodi katika kulipa mikopo ya wanufaika mkoani Kigoma
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Bregadia Jenerali Mstaafu Emmanuel Maganga akiwa katika picha ya pamoja Waajiri wa Mkoa huo na Watendaji wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...