Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Dkt Anna Mghwira pamoja na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro ,Hamis Issah wakipokea msaada wa mifuko 200 ya saruji kutoka kwa Mkurugenzi wa Kampuni ya Jun Yu , inayotengeneza saruji ya Moshi Cement ,Tian Haifeng . 

Na Dixon Busagaga wa Globu ya Jamii Kanda ya Kaskazini .

FAMILIA 400 za askari Polisi kati ya 1600 katika mkoa wa Kilimanjaro wanaishi uraiani hali inayochangia kupungua kwa maadili katika utendaji kazi kwa baadhi ya askari kutokana na kuishi maeneo yasiyokuwa kambi za Polisi.

Kutokana na hali hiyo tayari Jeshi la Polisi mkoa wa Kilimanjaro limeanza ujenzi wa nyumba sita katika eneo la kambi za Polisi mjini Moshi kwa ajili ya makazi ya askari hao baada ya kupokea kiasi cha Sh Milioni 150 zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ,Dkt John Pombe Magufuli.

Akizungumza wakati wa kupokea msaada wa mifuko 200 ya saruji kutoka kampuni ya kichina ya Jun Yu investment ,watengeneza wa saruji ya Moshi Cement ,Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro,Kamishna Msaidizi wa Polisi ,Hamis Issah alisema fedha hizo ni sehemu ya Sh Bilioni 10 zilizotolewa na Rais.

“Nimshukuru mh. Raisi wa Jamuhuri wa muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli kwa jitihada zake za dhati za kuboresha ustawi wa askari kwa kutoa shilingi Bilioni 10 kwa ajii ya kujenga nyumba za kuishi askari polisi na familia zao katika mikoa yote nchini.”alisema kamanda Issah.

“Aidha siku ya leo kwa niaba ya maofisa,wakaguzi na askari wa jeshi la polisi mkoa wa Kilimanjaro ,niushukuru uongozi wa kampuni ya Moshi Cement kwa kutupatia mifuko 200 ya saruji na huu ni mwanzo mzuri kwa wadau kuendelea kutusaidia.”alingeza Issah.

Kamanda Issah alisema uongozi wa kampuni ya Moshi Cement wamejitoa kuchangia baada ya kufahamu umuhimu wa jeshi la polisi katika shughuli zao za uwekezaji na pia katika kumuunga mkono Mh. Raisi wa jamuhuri ya muungano wa Tanzania ,Dkt Magufuli katika juhudi za kuboresha jeshi la Polisi.

“Nyumba hizi zinatakiwa zikamilike ifikapo Juni 31 mwaka 2019 hivyo tunajitahidi kuwashirikisha wadau wa jeshi la polisi na wadau wengine wapenda maendeleo ili kukamilisha ujenzi huu kwa wakati,na pia ikiwezekana tuongeze nyumba nyingine katika eneo hili .”alisema Kamanda Issah .

Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Dkt Anna Mghwira akizungumza mara baada ua kupokea msaada huo alisema ni jukumu la serikali kuhakikisha askari wake wanaishi kwenye maeneo yaliyo safi na salama huku akieleza kuwa shauku yake ilikuwa ni kuona ujenzi huo ni wa nyumba za Ghorofa.

“Nilipokuja kutembelea uwanja huu binafsi nilitamani sana kama tungekuwa tumejipanga haya majengo yangeenda Juu ili kuacha nafasi ya kutosha kwa ajili ya watoto wa askari na jumuiya inayoshi hapa ,kupata sehemu mbalimbali zikiwemo za mapumziko na biashara kidogo “alisema Dkt Mghwira.

Alisema ujenzi wa nyumba za Ghorofa zingetoa nafasi kwa askari Polisi kuishi maisha ya Staha wanapokuwa kambini tofauti na ilivyo sasa hali iliyowalazimu askari kuongeza vyumba katika nyumba wanazo ishi ili waweze kuenea na familia zao.

“Nilitamani sana msingi huu ungetengenezwa kwa ajili yakupanda juu lakini tukasema kwa sababu serikali imetupa fursa hii ebu tuitumie hii kuwa kichocheo kwa ajili ya makazi mengine yatakayo endelea yasibaki kuwa ya chini .” alisema Dkt Mghwira .

Kutokana na hali hiyo Dkt Mghwira alimuagiza Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro,Hamisi Issah kukaa na waandisi kwa ajili ya kufanya tathimini ya makazi yanayohitajika kwa ajili ya askari Polisi pamoja na gharama za ujenzi wa nyumba hizo.

“ RPC kakae na wahandisi waturetee utaratibu wa kujenga makazi yote yanayohitajika tukipandisha juu na tutahitaji fedha kiasi gani ,…tunaweza kuanza kukusanya kidogo kidogo kama hivi ninavyoona sasa,maana tunaweza tukamaliza ujenzi hata kabla hatujaigusa ile pesa iliyotolewa na Rais Magufuli.”alisema Dkt Mghwira .

“Na mimi kwa hili naomba niwahamasishe tena wana Kilimanjaro ,yeyote anaye jisikia kutenda lolote katika hili alete mchango wake kama sadaka yake kwa ajili ya maisha na ustawi wa askari wetu ,kama mnavyoona eneo hili liko wazi na linapakana na makazi ya watu na hakuna ukuta unaotenganisha maeneo hayo , hili ni upungufu mkubwa sana ,”aliongeza Dkt Mghwira.

Tayari hadi sasa wadau mbalimbali wameendelea kutoa michango yao ikiwemo kampuni ya Rocktronic iliyotoa Loli pamoja na Greda kwa ajili ya kusafisha eneo la ujenzi ,Ravj aliyetoa kokoto tani saba , mfanyabiashara Mr Ngowi aliyetoa mifuko 200 ya saruji pamoja na askari namba E 1708 Koplo Dickson Mwakabuta ambaye ametoa mchanga Lori moja kwa hiari yake.
Sehemu ya mifuko 200 ya saruji iliyotolewa na Kampuni ya Jun Yu inayoendeshwa na raia wa China iliyotolewa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za askari Polisi .

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Dkt Anna Mghwira ,akiongizwa na Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro ,Hamis Issah kwa kutizama maendeleo ya ujenzi wa nyumba za askari zinazojengwa katika kambi ya Polisi Moshi. 
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Dkt Anna Mghwira ,akizungumza jambo na Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro ,Hamis Issah mara baada ya kutizama maendeleo ya ujenzi wa nyumba za askari zinazojengwa katika kambi ya Polisi Moshi. 

Baadhi ya Mafundi wakiendelea na ujenzi katika eneo hilo la kambi ya askari Polisi. 
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro,Hamis Issah akizungumza wakati wa kupokea msaada wa saruji kutoka kampuni ya Jun Yu. 
Baadhi ya wageni waliofika katika hafla hiyo. 
Baadhi ya Raia wa China wanaoendesha kiwanda cha kutengeneza saruji wakiwa katika hafla hiyo. 

Mkurugenzi wa Kampuni ya Jun Yu , Tian Haifeng akimwaga maji wakati Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro,Dkt Anna Mghwira akinawa Mikono.
Dkt Mghwira akizungumza jambo na Mkurugenzi wa Kampuni ya Jun Yu , Tian Haifeng mara baada ya hafla fupi ya kupokea msaada wa Saruji kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za askari Polisi.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...