Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (wa kwanza kulia) akiwa katika kikao cha mwaka cha Majaji wa Mahakama ya Rufani cha kutathmini utendaji wa mwaka 2018 na kuweka malengo ya mwaka 2019. Kikao hicho kilifanyika kwa siku mbili (2) Aprili 23 na 24, 2019 katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Mwalimu Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam. Kikao hicho kimewashirikisha Wahe. Majaji wa Mahakama ya Rufani, Manaibu Wasajili wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu, Wasaidizi wa Kisheria wa Majaji, Makarani na Watunza kumbukumbu wa Mahakama ya Rufani.

Na Mary Gwera, Mahakama

JAJI Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewataka Manaibu Wasajili wa Mahakama Kuu nchini na wote wanaoshughulika na uandaaji wa kumbukumbu za rufaa kuzingatia sheria na kanuni muhimu katika uandaaji wa nyaraka hizo ili kuondoa mapungufu yanayoweza kusababisha usikilizaji wa rufaa kukwama.

Akizungumza wakati wa kufunga rasmi kikao cha siku mbili (2) cha Majaji wa Mahakama ya Rufani nchini kilichofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Mwalimu Nyerere (JNICC) Aprili 24, 2019, Mhe. Jaji Mkuu alisema kwa kufanya hivyo kutapunguza makosa yanayojitokeza ambayo kwa wakati mwingine hupelekea ucheleweshaji wa usikilizwaji wa rufaa hizo kwa kufanya marekebisho mara kadhaa.

“Ni vyema Manaibu Wasajili na Watumishi wanaohusika katika utayarishaji wa nyaraka hizo, kuandaa vyema kumbukumbu za rufaa ‘records of appeal’ kwa kuibua makosa mbalimbali yanayoonekana pindi wanapoandaa kumbukumbu za rufaa ili kuzuia kesi kuchukua muda mrefu Mahakamani,” alieleza Mhe. Jaji Mkuu.

Awali, akitoa taarifa ya Utendaji wa Mahakama ya Rufani kwa mwaka 2018, Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama ya Rufani (T), Mhe. Elizabeth Mkwizu alisema kwa mwaka huo Mahakama ya Rufani iliweza kushughulikia jumla ya mashauri 1230 katika jumla ya vikao 38 vilivyofanyika katika Kanda 11 kote nchini.

Mhe. Mkwizu alisema kuwa jumla ya Mashauri 1108 kati ya 1230 yaliyopangwa katika vikao hivyo yalimalizika ikiwa ni asilimia tisini (90%) ya mashauri yote yaliyopangwa kusikilizwa.

“Hiki ni kiwango kizuri pamoja na kuwa lengo la kumaliza mashauri kwa asilimia mia moja (100%) halikutimia, hata hivyo tunatoa pongezi kwa wote waliochangia mafanikio hayo,” alieleza Mhe. Mkwizu.

Akizungumzia muda wa mashauri kukaa Mahakamani, Mhe. Mkwizu alisema kuwa takwimu za mashauri zinaonyesha kushuka kwa wastani wa muda wa rufaa za jinai kukaa Mahakamani kutoka siku 5240 mnamo Februari, 2017 hadi siku 898 kufikia mwishoni mwa Desemba 2018 na kusema hii ni hatua kubwa.

Kwa upande mwingine, kwa mwaka huu 2019 Mahakama ya Rufani imejiwekea malengo ya kuendelea kusikiliza mashauri na kuimarisha masjala.

Kwa mujibu wa taarifa ya Mpango kazi wa Mahakama ya Rufani ya mwaka 2019 Mahakama ya Rufani tayari imepitia Rejista na kukusanya takwimu za mashauri, kufanya ‘stock taking’ ya mashauri yaliyopo katika masjala, kuainisha idadi ya mashauri yaliyopo kwa kanda na kwa umri lengo likiwa ni kuweka mkakati wa uondoshaji wa mashauri ya zamani kulingana na mzigo uliopo kwa kila kanda.

Mkutano wa mwaka huu wa Wahe. Majaji wa Mahakama ya Rufani pia uliwashirikisha Manaibu Wasajili, wasaidizi wa kisheria wa Majaji, Makarani na watunza kumbukumbu ambao walitoa taarifa za utendaji kazi pamoja na changamoto zinazowakabili ili waweze kusaidiana kwa pamoja kupanga mikakati ya kumaliza mashauri kwa wakati.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...