Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Mpango (Mb) kushoto, akiwa pamoja na Makamu wa Rais wa Shirika la Maendeleo la Japani-JICA, Bw. Hiroshi Kato, walipokutana na kufanya mazungumzo kwenye Ofisi za ubalozi wa Tanzania mjini Washington DC-Marekani, kando ya Mikutano ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la KImataifa-IMF
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Mpango (Mb) kushoto, akiwa pamoja na Makamu wa Rais wa Shirika la Maendeleo la Japani-JICA, Bw. Hiroshi Kato, walipokutana na kufanya mazungumzo kwenye Ofisi za ubalozi wa Tanzania mjini Washington DC-Marekani, kando ya Mikutano ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, ambapo JICA imeahidi kutoa ruzuku na mikopo yenye masharti nafuu ili kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo nchini Tanzania.

Na Benny Mwaipaja, WFM, Washington D.C

 Serikali ya Japan kupitia Shirika lake la Maendeleo la Kimataifa-JICA inakusudia kuipatia Tanzania mkopo nafuu pamoja na ruzuku wenye thamani ya zaidi ya dola milioni 345 za Marekani, sawa na takriban shilingi bilioni 794, kwa ajili ya kutekeleza miradi mitatu ya maendeleo ikiwemo ukarabati wa barabara ya Arusha hadi Holili, ukarabati wa Bandari ya Kigoma na Mradi wa Maji Safi na Usafi wa Mazingira Visiwani Zanzibar.

Ahadi hiyo imetolewa na Makamu wa Rais wa Shirika la Maendeleo la JICA anayesimamia Ukanda wa Kusini mwa Jangwa la Sahara Bw. Hiroshi Kato, alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, Mjini Washington D.C nchini Marekani.

Ameitaja miradi hiyo iliyoko mezani kwao inayosubiri kupatiwa fedha wakati wowote kuanzia sasa kuwa ni mradi wa ukarabati wa barabara ya Arusha-Holili utakaopatiwa mkopo wa dola milioni 221, Mradi wa maji safi na usafi wa mazingira Zanzibar utakaopatiwa fedha kupitia mkopo wa dola milioni 99 na mradi wa upanuzi wa Bandari ya Kigoma ambao Japan itatoa ruzuku ya dola za Marekani milioni 25.

Bw. Kato amesema kuwa Japan inajivunia ushrikiano wa muda mrefu kati yake na Tanzania na kwamba iko tayari kusaidia juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano za kuwaletea wananchi wake maendeleo na kuitaka Serikali kuwasilisha miradi yake ya kimkakati ambayo Japan itafadhili kupitia mikopo yenye riba nafuu pamoja na ruzuku.

Akizungumza na Mwakilishi huyo wa Japan katika Ubalozi wa Tanzania nchini Marekani, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, ameishukuru Japan kwa uhusiano wake mzuri na Tanzania na namna inavyo isaidia nchi kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo akitaja mmoja wa miradi hiyo kuwa ni barabara ya juu ya kwanza nchini Tanzania  katika makutano ya Tazara Jijini Dar es Salaam, maarufu kama Daraja la Mfugale.

Dkt. Mpango ameiomba Japan kupitia Shirika lake la JICA kutoa ruzuku na mikopo nafuu ili kutekeleza miradi ya kimkakati ya ujenzi wa reli ya kisasa kwa kiwango cha kimataifa - SGR, Mradi wa kufua umeme wa Rufiji, Ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Msalato mkoani Dodoma, ujenzi wa barabara za mzunguko jijini Dodoma, ujenzi wa mtandao wa barabara, upanuzi wa bandari na miradi mingine ya kijamii.

Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango anaongoza ujumbe wa Tanzania katika mikutano ya kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF, inayofanyika mjini Washington DC nchini Marekani, ambapo ametumia fursa hiyo kukutana na wadau wa maendeleo kupenyeza ajenda za maendeleo ya kiuchumi ya Tanzania.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...