Wasimamizi wa Uchaguzi kwenye Uchaguzi Mdogo wa Arumeru Mashariki na
Kata Sita (6) za Tanzania Bara unaotarajiwa kufanyika Tarehe 19 Mei
mwaka huu wametakiwa kuwa na weledi ili kuhakikisha uchaguzi unakuwa
huru na wa haki.
Akifungua mafuzo kwa wasimamizi hao Jijini Dodoma leo (Ijumaa Tarehe
12.04.2019), Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Mhe.
Jaji (Rufaa), Mbarouk Salum Mbarouk amewaambia wasimamizi hao kwamba
weledi utapatikana kwa kuzingatia sheria, kanuni, taratibu na
maelekezo ya Tume.
Jajji Mbarouk amewakumbusha kuwa Tume ndiyo yenye jukumu la kusimamia,
kuendesha na kuratibu Uchaguzi, lakini watakaosimamia jukumu hilo kwa
karibu ni wao (wasimaizi) kwa sababu wanabeba dhamana katika Jimbo
hilo na Kata hizo sita.
Aidha, kiongozi huyo aliwaambia kuwa wanapaswa kuhakikisha kuwa
wanazingatia maelekezo watakayopewa na Tume, kuzingatia matakwa ya
Katiba na Sheria zinazosimamia Uchaguzi badala ya kufanya kwa mazoea.
Pamoja na hayo, Jaji aliwaeleza Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi hao
kuwa wanapaswa kujiamini na kujitambua kwa sababu wameaminiwa na Tume
na wahakikishe kwamba wanayajua maeneo yao ya uchaguzi vyema.
Amesema chaguzi hizo ndogo zitajumuisha wapiga kura 211,741
waliojiandikisha Katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura katika vituo
567 vya kupigia kura.
Kaimu Mkurugenzi wa Uchaguzi, Bi. Givenes Aswile aliwakumbusha
washiriki hao wa mafunzo kuwa wanapaswa kuhakikisha kwamba chaguzi
hizo zinafanyika bila kuwa na dosari ili kupunguza malalamiko na
mashauri mahakamani.
Kaimu Mkurugenzi aliwakumbusha pia Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi
hao kuwa wanatakiwa kuwepo maeneo ya kazi muda wote katika kipindi cha
kutoa fomu za uteuzi, siku ya uteuzi, wakati wa kampeni, siku ya
kupiga kura, kuhesabu na kujumlisha kura hadi kutangaza matokeo ya
Uchaguzi.
Bi. Aswile aliwaambia kuwa wajiepushe na migogoro ya Vyama vya siasa
kwa kutotoa fomu za uteuzi kwa wagombea wawili wa Chama kimoja cha
Siasa. Kila Chama kinatakiwa kumdhamini Mgombea mmoja tu.
Wakati wa Kampeni, Kaimu Mkurugenzi aliwakumbusha kwamba wanatakiwa
kuunda Kamati za Maadili Ngazi ya Jimbo kwa Ubunge na Kamati ya
Maadili Ngazi ya Kata kwa Udiwani ili kushughulikia kwa haraka
malalamiko kama yatakuwepo.
Kata zenye uchaguzi ni pamoja na Uwanja wa Ndege iliyopo Halmashauri
ya Wilaya ya Mpanda Mkoani Katavi, Kitobo iliyopo Halmashauri ya
Wilaya ya Missenyi Mkoani Kagera, Kyela iliyopo Halmashauri ya Wilaya
ya Kyela Mkoani Mbeya, Mikocheni iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya
Kinondoni Mkoani Dar es Salaam, Mvuleni iliyopo Halmashauri ya Wilaya
ya Lindi Mkoani Lindi na Manda iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya
Chamwino Mkoani Dodoma.
Wajumbe wa Tume na Wasimamizi wa Uchaguzi Mdogo kwenye Jimbo la Arumeru Mashariki na Kata Sita (6) za Tanzania Bara utakaofanyika Tarehe 19 Mei mwaka huu wakifuatilia mada iliyokuwa ikiwasilishwa. Mafunzo kwa wasimamizi hao yamefanyika Jijini Dodoma leo (Ijumaa Tarehe 12.04.2019) chini ya uratibu wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC). (Picha kwa Hisani ya NEC)
Wasimamizi wa Uchaguzi Mdogo kwenye Jimbo la Arumeru Mashariki
na Kata Sita (6) za Tanzania Bara utakaofanyika Tarehe 19 Mei mwaka
huu wakila kiapo wakati wa mafunzo yaliyoandaliwa kwa ajili yao na
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Jijini Dodoma leo (Ijumaa Tarehe
12.04.2019). (Picha kwa Hisani ya NEC)
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...