*Abaini malipo hewa ya
mabilioni ya fedha, mashirika mengine hoi kwa madeni
Na Ripota Wetu, Globu
ya jamii
MDHIBITI na Mkaguzi
Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Profesa Mussa Asaad ametoa ropoti ya ofisi
yake kuhusu ripoti ya ukaguzi wa hesabu za Serikali ambapo imebaini uwepo wa
ubadhirifu wa fedha katika maeno mbalimbali.
Ripoti hiyo ya CAG ni
ile inayoishia kwa mwaka wa fedha ulioishia Juni 2018 ambapo Profesa Assad
anasoma ripoti hiyo leo kwa waandishi wa habari Mjini Dodoma ripoti hiyo
inaonesha mashirika ya umma 14 yenye yana matatizo makubwa ya kifedha na kwamba
baadhi ya mashirika yamepata hasara kiasi cha kusababisha madeni zaidi ya mitaji yao kwa zaidi ya
asilimia 100.
"Ukiangalia
ripoti hii inaonesha kati ya mashirika hayo 14, mashirika 11 yanajiendesha kwa hasara kwa
zaidi ya miaka miwili.Ni dhahiri mashirika hayo hayawezi kujiendesha bila
kutegemea msaada kutoka Serikali Kuu. Kwa mazingira ya aina hiyo mashirika hayo
hayaweza kujiendesha na kutoa huduma kwa jamii,"amesema.
Profesa Assad
ameyataja baadhi ya mashirika hayo ni Kampuni ya Maendeleo ya Nishati ya Joto
Tanzania (TGDC), Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA), Kampuni ya Ndege
Tanzania (ATCL), Baraza la Taifa la Bishara, Baraza la Michezo la Taifa, Mamlaka
ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira, Mtwara, Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa
Mazingira, Lindi na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira, Mwanza, Shirika
la Maendeleo ya Petroli (TPDC), Kampuni ya Usafirishaji na Ujenzi na Ukarabati
wa Miundombinu ya Usambazaji wa Umeme, Bodi ya Utalii Tanzania, Kampuni ya Simu
(TTCL – Pesa), Shirika la Maji Safi na Usafi wa Mazingira, Dar es Salaam
(DAWASCO) na Bodi ya Maziwa Tanzania.
Akizungumzia zaidi
ripoti hiyo, Profesa Assad amesema kuwa ripoti imebaini katika ununuzi wa
Mashine za Mfumo wa Kidigitali wa Usajili wa Wapiga kura (BVR) uliofanywa na
Tume ya Taifa ya Uchaguzi(NEC) ilinunua mashine za BVR, 8,000 ili kusajili wapiga
kura na kati ya mashine hizo 5,000 hazikukidhi vigezo vilivyoainishwa kwenye
mkataba.
Amesema kuwa hivyo imesababisha
kutolandana kimatumizi na vile vilivyonunuliwa hapo awali na Mamlaka ya
Vitambulisho vya Taifa (NIDA) na Wakala wa Taifa wa Usajili, Ufilisi, na Udhamini
(RITA). "Hivyo kutolandana huko kumeisababishia hasara kwa Serikali
Sh. milioni 862.08 zilizotumiwa na NIDA kununulia leseni mpya za “Windows” na
“Biometric Algorithms” ili kubadilisha mashine 5,000 zilizopokelewa kutoka NEC
ziweze kufanya kazi na mfumo wa BVR wa NIDA,"amesema.
Pia amesema ndani ya
ripoti hiyo imebaini mzabuni alilipwa dola milioni 72.3 badala ya dola milioni
72.1 na kwamba kiasi hicho kilikuwa bei ya mkataba."Ukifuatilia eneo hilo
utaona kuna ongezeko la dola 148,243.73. Wakati mafunzo kwa maofisa 15 wa
TEHAMA wa NEC hayakufanyika licha ya mzabuni kulipwa dola 358,650 kwa ajili ya
mafunzo hayo".
Wakati huo huo Profesa
Assad amesema ripoti hiyo imebaini ndani ya
Jeshi la Polisi katika
ununuzi wa sare za askari ambapo ukaguzi maalumu uliofanywa ndani ya jeshi
hilo,umeonesha Polisi wamelipa Sh.bilioni 16.66 bila ya kuwepo ushahidi wa
uagizaji na upokeaji wa sare za askari kwa Boharia Mkuu katika jeshi hilo.
Profesa Assad amesema ukaguzi
huo umebaini kuna maoni ya kisheria ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali yanayohusu
uwasilishaji wa kiapo cha nguvu ya kisheria na leseni halali ya biashara
hayakuzingatiwa wakati wa kusaini Mkataba Namba. ME.014/PF/2015/2016/G/30 Lot
2, uliohusu ununuzi wa sare za askari polisi.
Amefafanua zaidi
ripoti imebaini katika ukaguzi maalumu wa Mfumo wa Utambuzi wa Alama za Vidole
(AFIS)kuna mambo yameonekana ambayo ni mahitaji ya kitaalamu kutoka idara
inayotumia mfumo huo ambayo hayakuzingatiwa wakati wa kutathmini na kutoa
zabuni.
Pia amesema kuna
malipo ya Sh. bilioni 3.30 yalifanyika kwa mzabuni kwa ajili ya huduma ya
matengenezo na msaada wa kitaalamu wa Mfumo wa Utambuzi wa Alama za Vidole
kwenye mikoa nane ya Kipolisi ya Temeke, Simiyu, Mwanza, Tabora, Rukwa, Kigoma,
na Kinondoni Geita lakini Polisi
ilishindwa kuthibitisha kuwa matengenezo hayo na msaada wa kitaalamu
ulifanyika.
Profesa Assad amesema
kwamba vifaa vya Utambuzi wa Alama za Vidole vyenye thamani ya Sh. bilioni 1.73
havikufungwa kwenye magereza 35 yaliyoainishwa badala yake vilihifadhiwa katika
Ofisi ya Upelelezi, Makao Makuu ya Jeshi la Polisi na kuongeza malipo ya Sh.
milioni 604.3 kwa ajili ya mafunzo kwa wataalamu 30 hayakufanyika kwani Jeshi
la Polisi lilishindwa kuwaonesha maofisi ya CAG monita 58 za kompyuta aina ya
Dell zenye thamani ya Sh. milioni 159.1 zilizopelekwa kwenye Kitengo cha Uchunguzi
wa Kisayansi cha Makao Makuu ya Jeshi la Polisi.
"Ripoti inaonesha
kuwa monita 213 za kompyuta aina ya Dell zililipiwa Sh.milioni 195.22 kwa
mzabuni Lugumi Enterprises Limited lakini mzabuni hakuzileta,"amesema
Profesa Assad.
Kuhusu malipo hewa
,Profesa Assad amesema ripoti imebaini katika uchunguzi wa vitabu vya fedha,
taarifa za benki na hati za malipo za Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, kuna
malipo ya Sh. bilioni 3, kati ya malipo hayo sh. bilioni 2.61 yalikuwa malipo
hewa, sh. milioni 350.8 ni malipo ambayo walipwaji walishindwa kubainika na sh.
milioni 42.6 hazikuweza kuthibitika kupokelewa na walipwaji.
"Malipo hayo yalitakiwa
kulipwa watoa huduma za afya kwa kutumia hundi zilizofungwa lakini yalifanywa
kwa fedha taslimu kinyume na Kanuni za Fedha za Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya.Makusanyo
ya mwaka yanaendelea kuwa makubwa zaidi ya malipo ya huduma za bima ya afya,
ambapo kwa sasa malipo ya huduma za afya yanakua kwa uwiano mkubwa mwaka hadi
mwaka zaidi ya uwiano wa kukua kwa mapato,"amesema wakati anasoma ripoti
hiyo.
Ameongeza kutokana na
hali hiyo makisio ya madai ya huduma za bima ya afya pekee ifikapo mwaka wa
fedha utakaoishia Juni 2024 yatakuwa ni asilimia 99.2 ya jumla ya makusanyo
yote ambapo uwiano huu unakisiwa kuongezeka zaidi hadi kufikia asilimia 104.8
katika mwaka unaofuata. Profesa Assad amesema uchunguzi wa vitabu vya
fedha, taarifa za benki na hati za malipoza Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya umebaini
uwepo wa Sh.bilioni tatu.
"Kati ya malipo
hayo Sh.bilioni 2.61 yalikuwamalipo hewa, Sh. milioni 350.8 ni malipo ambayo
walipwaji walishindwa kubainika na Sh. milioni 42.6 hazikuthibitika kupokelewa na
walipwaji.
Kwa upande wa
udanganyifu katika halmashauri, Profesa Assad amesema kuna udanganyifu katika
malipo ya Sh. milioni 267.89 kwenye akaunti ya matumizi mengine katika
Halmashauri ya Wilaya ya Rombo ambapo alikagua malipo mbalimbali katika akaunti
ya matumizi mengine na kubaini kuwa kwa nyakati tofauti kuna watumishi
walianzisha, kupitisha, na kufanya malipo ya ya Sh. milioni 267.89 ambayo
hayakuwa na viambatisho husika.
"Na mengine
yalikuwa na viambatisho vyenye shaka.Upotevu wa mapato ya zaidi ya Sh. bilioni
3.4 katika Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’ ambapo mapitio ya mfumo wa
ukusanyaji wa mapato ya ndani umebaini upungufu ukiwemo wa halmashauri hiyo
kushindwa kuwasilisha vitabu 425 vya kukusanyia mapato.
"Mambo mengine
yaliyobainika ni upotevu wa mapato ya ndani ya Halmashauri ya sh. bilioni 1.04
yaliyokuwa yanakusanywa na mawakala, kutopatikana kwa nyaraka muhimu za
makampuni ya mawakala wa ukusanyaji wa mapato kwa mikataba yenye thamani ya sh.
bilioni 2.36 na malipo hewa ya sh. milioni 73.45 katika kandarasi za Programu
ya Maendeleo ya Sekta ya Maji katika Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’.
"Pia ukaguzi
maalumu umebaini kuwa fedha Sh. milioni 73.45 za Programu ya Maendeleo ya Sekta
ya Maji zililipwa kwa wakandarasi kama dharura bila kuwepo kazi za
dharura. Ukaguzi umebaini kutokuwepo kwa ushahidi wowote wa kufanyika kwa
kazi hiyo na hivyo kudhihirika kuwa matumizi hayo ni hewa," amesema
Profesa Assad.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...