Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi amesema
kuanzia sasa gharama za urasimishaji haitazidi shilingi 150,000 badala
ya 250,000 iliyopangwa awali na makampuni yatakayoenda kinyume
yatachukuliwa hatua ikiwemo kufutwa.
Lukuvi alitoa kauli hiyo leo jijini Dar es Salaam alipokutana na
Makampuni ya Upangaji na Upimaji yanayofanya kazi ya urasimishaji
katika mitaa mbalimbali nchini pamoja na watendaji wa sekta ya ardhi.
Kwa mujibu wa Lukuvi, baada ya Wizara yake kuona zoezi la urasimishaji
linasuasua wamegundua asilimia 30 pekee ndiyo iliyorasimishwa tangu
kuanza zoezi hilo na hali hiyo imechangiwa na uwezo mdogo wa wananchi
wengi kumudu gharama za urasimishaji.
Waziri Lukuvi alisema, alichotegemea kwa makampuni yaliyopewa kazi ya
urasimishaji ni kuwa na uzalendo kwa kushusha gharama lakini
yameshindwa kupunguza gharama jambo lililoifanya serikali kuona haja
ya kupitia upya gharama hizo na kubaini gharama za msingi ili
kumuwezesha mwananchi kupata hati na kusisitiza punguzo hilo
halitawahusu waliolipia gharama za urasimishaji.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi ameyataka makampuni
yanaoyoendesha zoezi la urasimishaji kuhakikisha kiasi cha fedha
inachowatoza wananchi kinaishia hatua ya Hati na gharama itakayolipwa
na mwananchi baada ya kurasimishwa ni kodi ya ardhi na
kuyatahadharisha kutochukua muda mrefu kukamilisha zoezi hilo.
Amewataka wananchi wote wanaoishi kwenye maeneo yasiyo rasmi
kuhakikisha wanaingia katika zoezi la urasimishaji ili kupata hati
itakayowawezesha kiuchumi na kusisitiza kuwa suala hilo linafanyika
kwa nia njema kwa nia ya kuwaongezea mtaji wananchi kwa kupatiwa
nyaraka itakayowasiadia kukopa fedha benki.
Akigeukia suala la Leseni za Makazi, Waziri Lukuvi alisema zoezi hilo
linaendelea vizuri katika jiji la dar es Salaama kwa gharama ya
shilingi elfu tano hadi hatua ya upatiwaji leseni ya makazi na
kusisitiza kuwa leseni hiyo siyo ya kudumu bali itakuwa kwa miaka
mitano na kuwataka wananchi walio katika maeneo ya urasimishaji
kuendelea na zoezi hilo kwa kuwa wizara inayo kanzi data itakayotunza
takwimu za mazoezi yote mawili.
‘’Tunataka kuwa na database ya nani anamiliki ardhi kiasi gani na kila
mwananchi lazima awe na leseni ya makazi au hati kwa lengo la
kushiriki kulipa kodi’’ alisema Lukuvi
Hata hivyo, Lukuvi alisikitishwa na baadhi ya Makampuni ya
urasimishaji kushindwa kutoa takwimu wakati wa zoezi la upimaji
zinazoendana na miongozo ya wizara na kuyataka yote yaliyoenda kinyume
kurudia zoezi na kuongeza kuwa kuna makampuni 34 yaliyotuma takwimu
ambazo ni chafu na kuyapongeza makampuni mawili ya Visible Planners na
Afro Max kwa kufuata taratibu zote za urasimishaji.
Lukuvi alionya baadhi ya makapuni ya urasimishaji kuacha kuwalaghai
wananchi kwa kuwapatia leseni za makazi badala ya hati kwa gharama za
urasimishaji na kusema kufanya hivyo ni kosa la uhujumu uchumi na
hatua kali zitachukuliwa dhidi yao.
Vile vile Lukuvi amewataka watendaji wa serikali ambao wana makampuni
yanayofanya kazi ya urasimishaji kuchagua jambo moja la kuitumikia
serikali ama makampuni yao kwa kuwa wanatumia muda mwingi kufanya kazi
katika makampuni yao badala ya kuitumikia serikali.
‘’Ninyi watendaji wa serikali badhi yenu mna makampuni ya urasimishaji
na ndiyo mnaoharibu zoezi mnataka squatters ziendelee ili mnufaike na
mnapima halafu michoro mnapitisha ninyi hii ni conflict of interest’’
alisema Likuvi.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...