*Amwambia aache kuliita Bunge dhaifu na kama.analipenda basi ajiite yeye

*Amshauri ajipime,ajitafakari na ikiwezekana aende kwa Rais kujieleza...kisha ajiuzulu
*Asisitiza Bunge halitafanya kazi naye ila ripoti ya CAG sawa...amshangaa kuwaona wengine Mbuzi


Na Said Mwishehe,Globu ya jamii

SPIKA wa Bunge Job Ndugai amesema hawana tatizo na ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali(CAG) na kwamba wataifanyia kazi lakini msimamo wao Bunge halitakuwa tayari kufanya kazi na Profesa Mussa Assad.

Ameongeza kuwa amemsikia Profesa Assad akisema ataendelea kutumia kauli ya Bunge dhaifu,hivyo amemtaka afahamu kuwa hawataki kusikia Bunge linaitwa dhaifu na kama analipenda basi ajiite yeye dhaifu na sio Bunge.

Spika Ndugai amesema hayo leo Aprili 14,2019 wakati anazungumza na waandishi jijini Dar es Salaam ambapo pamoja ametumia nafasi hiyo kuelezea hawana tatizo na ripoti ya CAG lakini tatizo ni mtu ambaye ni Profesa Assad ,hivyo amemtaka ajitafakari,ajipime na ikiwezekana aende kwa Rais.

"Anapokwenda kwa Rais wala asione tabu kumwambia anajiuzulu.kama Bunge hatutafanya kazi na Profesa Assad atafanya kazi na nani?Aniambie au niambieni waandishi wa habari kama yupo anayeweza kufanya naye kazi,"amsema Spika Ndugai.

Ambapo amefafanua katika nchi nyingine Bunge likiadhimia kuhusu mtu hakuna njia nyingine zaidi ya kujiuzulu na kuchelewa kwake kujiuzulu anampa kazi Rais.

Spika Ndugai amesema kwamba Rais ni sehemu ya Bunge kwani yeye ndio kila kitu na hata bajeti zinazojadiliwa vipi na zikakosa saini ya Rais bado haijawa bajeti.

Amesisitiza Profesa Assad ameahidi kuendelea kutumia kauli ya kwamba Bunge dhaifu lakini amemtaka afahamu akiendelea watamuita na kumhoji tena na hiyo itakuwa mbaya zaidi kwake.

" Ujue kama mtu anakwambia usimuite hilo jina halafu wewe unang'ang'ania kumuita,kama analipenda asijiite yeye mwenyewe.Sisi hatutaki kuitwa dhaifu,halafu sijui alifikiria ,mule ndani kuna viongozi wa ngazi mbalimbali hadi Waziri Mkuu na mawaziri.Kuisema Bunge dhaifu maana yake anataka kuiambia Serikali ni dhaifu.Yaani hapa ni sawa na kumtukana mtu anayekupa chakula,"amesema Spika Ndugai.

Hata hivyo amesema yeye amesoma Norway na juzi hapa alikuwa Sweden ambapo mmoja ya marafiki zake alimwambia tatizo la Watanzania akisoma anajiona yeye ni ndio yeye na kuona wengine si chochote ,kumbe sio sawa.

Amesema kuwa Profesa sio kigezo cha kuona wengine ambao si maprofesa ni sawa na mbuzi,hivyo anatakiwa kutambua wabunge walioko Bungeni ni wawakilishi wa wananchi,wanao uwezo wa kuchuja,kuchambua na kujadili mambo kwa maslahi mapana ya nchi.

" Profesa Assad amefanya kosa na hapaswi kutukana Bunge kwa lugha za reja reja kwani Bunge linafanya mambo yake kwa mujibu wa kanuni za kibunge na si vinginevyo.Neno dhaifu linatumiwa na mhasibu anapofanya ukaguzi wake na baada ya hapo anakabidhi ripoti ambayo mwisho itakwenda kwadau.Na Bunge sasa ndio wanajadili kupitia kamati za Bunge kisha inaandaliwa taarifa na baada ya hapo ndipo yanapotolewa maagizo ya kuishauri Serikali.

"Ieleweke Bunge ndio chombo pekee ambacho kinaweza maagizo au mapendekezo ya kuishauri Serikali kuhusu ripoti ya CAG.Ndugu zangu waandishi katika hili neno analilotamka rafiki Assad hata alipoitwa kwenye kamati alishindwa kuthibitisha kwani Bunge lilitoa kamusi zote hadi za Kenya na neno dhaifu halina maana hiyo ambayo yeye amekuwa akitoa kwa Bunge.

Pamoja na hayo.ametumia nafasi hiyo kuwahakikishia Watanzania kwamba Bunge lao liko imara na litaendelea kufanya kazi,huku akifafanua ripoti ya CAG ambayo tayari iko mezani kwao itafanyiwa kazi chini ya kamati na baadae kujadiliwa.

Alipoulizwa kuhusu Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto kutumia fedha nyingi na sehemu kubwa zikionesha kutumiwa katika matibabu ya Spika ,amejibu kuwa kupanga matibabu sio jukumu lake ila tatizo litakuja iwapo fedha zimetumika vibaya.

Hata hivyo amesema yeye kama Mtanzania haoni tatizo Serikali kumtibu kwa lengo la kuokoa maisha yake kwani inafanya hivyo kwa watanzania wengi ambao ni malofa kama yeye(Ndugai)."Kosa langu ni kutibiwa au ilitakiwa ndio waseme.

"Kwanza kinachoonekana ni kitafuta sababu tu,hayo matumizi ya fedha kwa ajili ya Spika ziko ukurasa wa ngapi? niambieni?Tena mimi nilianza kuumwa mwaka 2015-2016 baada tu ya kuwaapisha wabunge.Hii ripoti ambayo imewasilishwa ni ya mwaka 2017-2018.Haya niambieni na bora nimeeleza maana wanataka kuaminisha watu uongo,"amesema.
Spika wa Bunge Mhe. Job Ndugai akizungumza na Waandishi wa Habari Ofisi Ndogo ya Bunge Jijini Dar es Salaam kuhusu ripoti ya Ukaguzi wa Hesabu za Serikali kwa mwaka 2017/18 .

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...