Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Godfrey Mbawala akizungumza na madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Hospitali kuu ya jimbo la Shandong la nchini China walipotembelea taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam.

Na Zawadi Masinde - JKCI

24/04/2019 Madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Hospitali kuu ya jimbo la Shandong nchini China wanatarajia kuja nchini mwezi wa nane mwaka huu kwa ajili ya kufanya kambi maalum ya matibabu ya moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Makubaliano hayo yamefikiwa leo katika kikao cha pamoja cha viongozi kutoka Hospitali hiyo na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kilichofanyika jijini Dar es Salaam..

Akizungumza katika kikao hicho Kiongozi wa msafara huo Wang Zhifeng alisema wataalamu hao ambao watakuja nchini watafanya upasuaji wa moyo wa kufungua na bila kufungua kifua pia watabadilishana ujuzi wa kazi na wenzao wa JKCI “Wataalamu wetu kutoka Hospitali ya Shandong wakija hapa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete watakuja na vifaa tiba ambavyo watavitumia katika upasuaji watakaoufanya. Pia mtatuambia ni vifaa gani vingine ambavyo mnavihitaji ili wataalamu wetu watakapokuja waje navyo”, alisema Zhifeng.

Aliendelea kusema kuwa kabla ya kuja kwa wataalamu hao hapa nchini kutaanza na program ya madaktari, wauguzi, wataalamu wa usingizi, mafundi sanifu wa moyo na Wahandisi wa vifaa tiba kwenda katika Hospitali hiyo kwa ajili ya mafunzo ya muda mfupi ya magonjwa ya moyo na mashine za moyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Prof. Mohamed Janabi aliwashukuru viongozi hao kwa kutembelea Taasisi hiyo na kusema kuwa kuja kwa wataalamu hao ni matokeo ya mkataba wa mahusiano uliosainiwa mwezi wa nane mwaka jana.

Makubaliano yaliyosainiwa katika mkataba huo ni kutolewa kwa mafunzo ya muda mfupi kwa madaktari, wauguzi, mafundi sanifu wa moyo na wahandisi wa vifaa tiba, kujenga jengo jipya la Taasisi hiyo, kutoa msaada wa vifaa tiba na kufanya kambi maalum za matibabu ya moyo ambazo zitasaidia kuwajengea uwezo wataalam wa hapa nchini.

Naye Mratibu wa ushirikiano wa Tanzania na China katika sekta ya Afya Dkt. Ligile Vumilia alisema makubaliano yaliyofikiwa katika kikao hicho ni lazima yafanyike kwa wakati na kwa manufaa ya nchi kwani hakuna Taasisi itakayotoa matibabu ya moyo zaidi ya wataalamu waliopo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete.

Hospitali kuu ya jimbo la Shandong inautaalamu wa hali ya juu wa kutibu magonjwa ya moyo ikiwa ni pamoja na kufanya upasuaji wa kufungua na bila kufungua kifua ambapo kwa mwaka 2018 ilifanya upasuaji wa moyo kwa wagonjwa 85,000.
Daktari wa magonjwa ya moyo kwa watoto kutoka Hospitali kuu ya jimbo la Shandong la nchini China anayejitolea katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Zhao Lijian akiwaelezea madaktari wenzake kutoka China namna ambavyo anatoa huduma ya matibabu ya moyo kwa watoto walipotembelea taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akizungumza na madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Hospitali kuu ya jimbo la Shandong la nchini China walipotembelea taasisi hiyo na kuahidi kushirikiana na taasisi hiyo kuboresha sekta ya afya ikiwemo afya ya moyo leo Jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi (katikati) akipokea zawadi ya picha ya Shandong kutoka kwa kiongozi wa madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Hospitali kuu ya jimbo la Shandong la nchini China Wang Zhifeng walipotembelea taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam na kuahidi kuendelea kushirikiana na taasisi hiyo katika kubadilishana ujuzi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi katika picha ya pamoja na menejimenti ya taasisi hiyo na madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Hospitali kuu ya jimbo la Shandong la nchini China walipotembelea taasisi hiyo na kuahidi kuendeleza ushirikiano katika sekta ya afya ikiwemo magonjwa ya moyo leo Jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akifafanua jambo alipokua akizungumza na madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Hospitali kuu ya jimbo la Shandong la nchini China walipotembelea taasisi hiyo na kuahidi kuendeleza ushirikiano katika kutoa huduma za matibabu ya moyo leo Jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Upasuaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Angela Muhozya akielezea namna idara ya upasuaji inavyofanya kazi alipokua akizungumza na baadhi ya madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Hospitali kuu ya jimbo la Shandong la nchini China walipotembelea taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam. Picha na: JKCI.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...